HAMMO GIZANI: MMEKUWA WANA WA NURU NA WANA WA MCHANA (SURA YA 6)
Neema
na iwe kwenu na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo.
Ewe
Muumba na Muumbuaji, twanyenyekea mbele zako tukishukuru kwa yote
unayotuwezesha siku baada ya siku. Katika mema au mabaya, Ewe, wabaki kuwa
Mungu na Bwana wa maisha yetu na katika yote twakuomba Ewe, Karima utujalie
kujua kusudi lako ili tutimize mapenzi yako maishani mwetu siku zote. Kwa hiyo,
Mungu Baba, tuzidishie uwepo wako maishani mwetu na utushindanie tunapozidiwa
kwa kuwa hatima ya maisha yetu i-mikononi mwako. Amina.
Wapendwa,
natumai sote tuwazima na kuwa twazidi kupambanua nyakati tukitumia Neno
Takatifu na kwa kumwuliza yeye aliyezifanya nyakati zote kwanzia mwanzo hadi
mwisho atufunulie makusudi yake na kutuongoza maishani. Maana, pasi na kufamu
Biblia Takatifu pamoja na kujipeana kwake Mola kwa dua, hatutaweza kuimarika
kiimani wala kushinda giza inayozidi kugubika mioyo ya wanadamu siku kwa siku. Kumbukeni
wale wanawali kumi na jinsi tano kati yao licha ya kujua Neno hawakujitayarisha
ipasavyo kumpokea Bwana harusi (Bw. Yesu). Taa (Neno) walizibeba sawa na wenzao
lakini hawakutwaa mafuta (Roho Mtakatifu) pamoja na taa zao, ila walitegemea
kuwa fahamu zao wenyewe na matendo yao pekee yangetosha kuwafanya wakubalike
mbele za Bwana, jambo ambalo Biblia Takatifu yatufunza haliwezekani kamwe. Upambavu
wao ni sawa na mtumwa yule aliyepewa talanta (kipawa cha Roho) moja na badala
ya kuitumia kama wenzake walivyofanya na kuchuma faida kwa niaba ya Bwana wao,
yeye aliamua kuizika na baadaye akamrejeshea Bwana wake ikiwa iyo hiyo moja aliyopewa,
(1KOR. 15:50; TIT. 3:5-7).
Na
wenzake walipozawadiwa kwa ajili ya wema na uaminifu wao, yeye alikaripiwa kwa
ukali na kunyang’anywa ile moja aliyokuwa nayo na kutupwa nje gizani kwenye
kilio na kusaga meno. Lakini kabla hayo kumfika, kwanza alijitokeza pamoja na
wenzake mbele za Bwana wao mara tu aliporudi toka safari ya siku nyingi
nakutaka kufanya hesabu ya mali yake. Hapa nitarudi nyuma kidogo na
kuwakumbusheni kuwa Bwana huyu si mwingine ila ni Kristo Yesu mwenyewe, na kama
Bwana ni Yesu Kristo kama tulivyoona wiki jana, basi, safari hii ya siku nyingi
sio nyingine ila ni kule kuchukuliwa kwake juu mbinguni baada ya kufuka kwake,
na kurejea kwake toka huko ndiyo twasubiri, sisi ambao ni watumwa wake (MDO.
1:10-11). Tukirudi kwake yule mtumwa aliyepewa talanta moja, twaona sababu ya
kukataliwa kwake ilikuwa ni upambavu aliotenda kwa kumrejeshea Bwana wake
talanta ile ile aliyopewa. Fauka ya hayo, alimlaki Bwana wake kwa kumzomea, ati
ni mtu mgumu anayevuna asipopanda na kukusanya asipotawanya, yaani, ni kana
kwamba mtumwa huyu hana akili razini kumjulisha talanta aliyonayo mkononi nani
kampa! Akaongeza kusema, “basi nikaogopa, nikaenda nikaificha talanta yako katika
ardhi tazama, unayo iliyo yako.” Matamshi haya yanatufunulia wazi wazi moyo wa
mtumwa huyu, jinsi alivyo mdharau Bwana wake na kumchukulia kama mtu asiyefaa
lolote.
Nitakuulizeni,
je, si haki ya mtumwa kumtumikia Bwana wake kwa utimilifu? Na akiwa ni mtumwa
mwenye busara, inamfaa kujituma zaidi wakati Bwana wake hayupo ili ahifadhi
imani na sifa nzuri alizonazo mbele za Bwana wake. Basi tafakari; itakuwaje baada
ya Bwana kuwadhamini watumwa wake kiasi cha kuwagawia mali zake kama mtu afanyavyo
na mwanawe na baadaye atakapotaka hesabu ya kazi zao, ajitokeze mmoja kati ya
watumwa wale na aanze kumzomea Bwana yule licha ya ukarimu wake na tena kwa
dharau amrudishie kile kile alichopewa, huku akidai kuwa Bwana wake huvuna
asipopanda! (hukumu nakuachieni). Ila ni dhahiri kuwa mtumwa wa aina hiyo
amefarakana kabisa na Bwana wake na wala hakuwezi tena kuwa na maelewano yoyote
baina yao. Ama kweli Bwana yule anadhihirisha kusudi la moyo wake kwa kuwapokeza
watumwa wale wema na waaminifu mali nyingi zaidi kuliko hapo kwanza na hata
kuwakaribisha katika furaha yake. Huku kukaribishwa katika furaha ya Bwana wao
sio kwingine ila ni kuwafanya warithi wa mali zake, yaani, wanatolewa utumwani
na kufanywa sawa na mwana halisi wa Bwana Yule, kwa kuwa ni mwana pekee ndiye
huwa na haki ya kushiriki furaha ya Babake wala sio watumwa, (EBR.1: 1-14).
Fika
hapa twaona kuwa sawa na wanawali wale wenye busara, watumwa hawa wema na
waaminifu wanakaribishwa na Bwana waingie katika furaha yake. Kukaribishwa kule
harusini na huku kukaribishwa kwa katika furaha ya Bwana wao ni mamoja. Kwani katika
mifano yote miwili; Bwana ni Kristo Yesu na watumwa hawa sawa na wanawali wale ni
waumini. Tena katika mifano yote miwili Bwana yule anakawia muda mrefu akiwa
mbali; kwenye mfano huu wa Talanta, anachukua siku nyingi safarini, na katika
mfano ule wa Wanawali Kumi, anachelewa sana kufika harusini. Vile vile katika
mifano yote miwili Bwana anapowasili kuna wale wanaopata kibali na kukubalika
mbele zake na kuna wale wanaokataliwa na hata kufukuzwa, na wale
aliowakaribisha katika furaha/sherehe yake ni wale waliompendeza kwa kushika
maneno yake na kutenda yaliyokubalika wakati wote ule Bwana wao alikuwa mbali
nao. Je, mpendwa unajitahidi kutenda matendo yatakayokubalika mbele za Bwana
wetu, ili atakaporudi upate kibali mbele zake na akukaribishe katika
furaha/sherehe yake, (KOL. 1:9-12).
Tofauti
na hao waliokubalika tunaona pia kuna wale waliokataliwa, katika mfano huu wa
Talanta ni mtumwa yule aliyepewa talanta moja na kukataa kuitumia talanta ile,
sababu ikiwa mtazamo wake duni kwa Bwana wake; ati alimjua kuwa mtu mgumu
anayevuna asipopanda! Je, Mkristo mwenzangu mtazamo wako ni upi kuhusu Bwana
wetu Yesu Kristo, na kama huna uhakika, (YER. 29:11-13; YN. 10: 7-10). Na
kwenye mfano ule wa Wanawali Kumi, sababu ya wale tano wapumbavu kukataliwa
ilikuwa ni kutegemea matendo yao licha ya kujua Neno, na kwa mujibu wa Neno hilo
kutarajia kuchelewa kwake Bwana harusi ila hawakujitayarisha sawa na lile Neno.
Na Bwana harusi alipochelewa (majaribu) kufika walisinzia na kulala (tumaini lao
likazima kabisa) hadi waliposikia amewasili ndipo wakaanza kuhangaika jinsi
watamlaki. Wanawali hawa wapumbavu sawa na mtumwa huyu walifungiwa nje kwenye
giza na huko ndiko kutakuwa na kilio na kusaga meno. Tazama kuwa kule nje si
ziwa la moto liko, yaani, hukumu hii inayowafika hawa wapumbavu si ile hukumu
ya KIYAMA bali ni hukumu tofauti, hukumu hii ni ile itwayo hukumu ya SIKU YA
BWANA, (SEF. 1:14-18; UFU. 6:12-17). Hukumu hii ni ile itakayotekelezwa duniani
kote baada ya Kristo Yesu kuwachukuwa watakatifu wake, na kutamatisha kipindi hiki
cha Madhila.
No comments:
Post a Comment