HAMMO GIZANI: MMEKUWA WANA WA NURU NA WANA WA MCHANA (SURA YA 5)
Neema
na iwe kwenu na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo.
Ewe, Muumba wa mbingu, dunia na
ulimwengu wote, twaliiuna Jina lako tukufu na takatifu lililojaa uweza, na kukushukuru
kwa wema na rehema zako maishaini mwetu. Ewe, Mungu uishie milele, twanyeyekea
mbele zako tukiomba utujalie uwepo wako maishani mwetu na uweza wako katika
yote yanayotukabili. Pia twakuomba utuzidishie rehema zako siku kwa siku kwa
kuwa tuwakosaji, viumbe dhaifu ambao msingi wetu ni udongo sawa na fahari yote
ya maisha yetu. Ewe, mwingi wa subira, tuongoze kwa neema na utufahamishe njia
zako ili tuzipitie siku zote na kwa mwenendo wetu kulifanya Jina lako kutukuzwa
na watu wote daima. Amin.
Wapendwa wa Kristo Yesu, kama
ilivyo kawaida yetu tukishajipeana kwake Mungu Baba, nakuziendeleza sifa zake twazama
katika kuangaza Neno Takatifu ili tuimarishe imani yetu kwa kujifahamisha
mapenzi yake Bwana wetu kwetu sisi tunaotumai kumwona ana kwa ana siku isiyo
mbali. Mungu Baba kwa mapenzi yake mwenyewe aliridhia kutupatanisha naye tena
kwa ukombozi mkuu; ukombozi uliofanyika kwa kifo cha Mwana wake wakipekee Yesu
Kristo. Na kwa kumwamini Yesu Kristo twapewa uweza wa kuwa wana wa Mungu, na
warithi wa ufalme wake pamoja na Kristo Yesu aliye Mkombozi na Mwokozi wa
wote. Yeye ndiye tunasubiri kufunuliwa kwake kama alivyotueleza ili tuwe pamoja
naye milele hata milele. Kufunuliwa huku kukaribu mno na inatubidi tujitahidi
kulijua Neno lake na kulishika kabisa ili siku itakapofika tusiwe wa kutahayari
na kuachwa nyuma kama wale wanawali wapumbavu.
Ni hapo wiki jana tulichambua mfano huu wa
wanawali kumi, katika uchambuzi wetu tuliona jinsi Bw. Yesu alivyoutumia kuwaeleza
wanafunzi wake kwa mafumbo kuhusu kufunuliwa kwake. Dhamira yake ikiwa kuwapa
tumaini la kweli kuwa watamwona tena na kuishi pamoja naye daima milele. Hata
sisi tuliopo leo hii tuwashiriki wa tumaini ile sawa na wale waliomsikiliza
aliponena mfano huu. Na kwa hakika utakubaliana nami kwamba kwa ukubwa shabaha
yake Bw. Yesu alipotabiri kuja kwake kupitia mfano huu, ilikuwa ni sisi
Wakristo tuishio katika nyakati hizi za mwisho, sawa na mfano unaoufuata wa
Talanta, (MAT. 25:14-30). Mfano huu wa Talanta ndiyo tutaangazia katika somo letu la wiki hii. Na kwa kifupi, mfano huu unatueleza kuhusu Bwana mmoja aliye waita
watumwa wake na kuwakabidhi mali zake; kila mmoja kwa kadiri ya uwezo wake,
kisha Bwana huyo akafunga safari ya siku nyingi. Halafu muda mrefu ulipokwisha Bwana yule alirejea na
kufanya hesabu ya mali aliowapa watumwa wake na kuwazawadia kila mmoja kwa
kadri ya bidii yake. Ila tofauti na mfano wa wanawali, baada ya kuumaliza mfano huu Bw. Yesu, aliongeza maelezo yaliyofafanua mafumbo yake. Katika kufafanua mfano huu anaelezea vile Mwana wa Adamu atakavyokusanya mataifa mbele zake na kuwabagua, huku
akiwakaribisha wale awaitao kondoo, waurithi ufalme wa Mungu na kuwafukuza wale
awaitao mbuzi na kuwatupa katika moto wa milele.
Kabla hatujazama zaidi
katika majadala wa leo ni vema kukumbuka kuwa mfano huu wa Talanta ndiyo
unatamatisha jibu lake Bw. Yesu alipowajibu wanafunzi wake swali lao walipomwomba awajuze ni nini itakuwa dalili ya kuja kwake na ya mwisho wa dunia.
Kwa hiyo, upambanuo wowote wa mfano huu lazima uwiane na maelezo yale mengine
ambayo Bwana alitangulia kuwaeleza wanafuzi wake kuhusu ni nini itakuwa dalili
ya kuja kwake na ya mwisho wa dunia. Sababu ya kusema hivi ni kuwa mfano huu
hutumika visivyo, ususan, kuwatia vijana motisha kutambua talanta zao na kuzitumia kama njia ya kujinasua na umasikini kwa kujitafutia
riziki pasi na kutegemea kazi za kuajiriwa. Sisemi kuwa hivi ni vibaya, la, ila
nasema kuwa uelewa huo hauwiani na madhumuni yake Bwana wetu, ikizingatiwa
swali alilokuwa akijibu aliponena mfano huu.
Natuutazame mfano wenyewe: Mfano
unaazia mstari wa kumi na nne kwa maneno, ‘Maana ni mfano wa mtu atakaye
kusafiri,’ swali la kujiuliza hapa ni, nini hiki ambacho kinafananishwa? Nalo
jibu lake twalipata katika aya iyo hiyo katika mstari wa kwanza, ‘Ndipo ufalme
wa mbinguni utafanana na,’ kwa mujibu wa mstari huu ni bayana kuwa Bw. Yesu, anaendeleza jibu lake kwa swali la wanafunzi wake na ndiyo maana haoni
haja ya kujirudia neno kwa neno anapoanza kuwasimulia mfano huu. Naye mtu huyo
atakaye kusafiri si mwingine ila ni Yesu Kristo mwenywe, na hili twajua kwa
mujibu wa maelezo yale aliyoyatoa mara tu alipomaliza kusimulia mfano huu wa
talanta; mstari wa thelathini na moja. Ila kwa wale watakao ushahidi zaidi
kwamba Bw. Yesu ndiye mwana wa Adamu, someni; (MAT. 8:20; 12:6-8; 13:41-43, LK.
19:9-10;). Nao, watumwa wale wanatuashiria sisi tuliookoka kwa kumwamini Bwana
Yesu Kristo; hapa najua kuna wale watakaouliza itakuwaje Bwana atufananishe na
watumwa? Ee, kwa kweli jambo hili si la kushanganza wala kudunisha kwani hata Mitume walipenda
kujitambulisha kama watumwa wa Kristo Yesu hasa Mtume Paulo, (RUM. 1:1). Nazo
mali walizopewa kila mtu kadiri ya uweza wake za ashiria vipawa Vya Roho Mtakatifu
ambavyo Bwana humgawia kila moja kwa hekima na mapenzi yake, (RUM. 12:1-9).
Japokuwa tushaona kuwa ni Bwana
atukirimiaye vipawa kwa hekima na mapenzi yake. Ningependa tutazame mstari wa kumi
na tano kwa makini zaidi, “Akampa mmoja talanta tano, na mmoja talanta mbili na
mmoja talanta moja; kila mtu kwa kadiri ya uwezo wake; akasafiri.” Kwa mujibu
wa mstari huu, kwanza aliwapa mali (vipawa) kisha akasafiri, walakini, kama
tujuavyo vipawa vya Roho vilitambulikana baada ya Pentekoste; siku ambayo Roho
Mtakatifu alishuka kama ndimi za moto nakutua juu ya vichwa vya Mitume (MDO.
2:1-4). Je, tutasema kuwa Bw. Yesu alikosea ama hakutilia manani maneno yake
alipozungumza vile? Tukumbukeni kuwa kile Bw. Yesu anachokifanya hapa ni
kutabiri na hata kama ni kwa mafumbo, matukio ya mambo yale yatakapotimia
lazima yafuate utaratibu ule. Na kwa kuwa baadhi ya mambo yale yalitimia muda
mfupi baadaye, twajua kwa uhakika kuwa yalitendeka sawa na utaratibu wa unabii huu. Kwani kabla ya Pentekoste Bw. Yesu alitangulia kuwabatiza wanafunzi wake kwa
Roho Mtakatifu kwa kuwavuvia na kuwaambia, “Pokeeni Roho Mtakatifu,” (YN. 20:22).
Basi tutasemaje kuhusu yaliyotukia siku ya Pentekoste! Yaliyotukia siku hiyo ya
Pentekoste yalithibitisha aliyokuwa tayari ameyatenda Bwana, (MDO. 1:6-9). Hali
kadhalika, lazima kila Neno katika Biblia Takatifu litimie kadiri ya utaratibu wa
vile ambavyo Neno lile lilinenwa, isitoshe, hata wewe mpenzi wa Mungu kama alikuahidi
jambo subiri tu, maana, lazima litatimia sawa na Neno lake, hata kama matukio yanayokukabili hayaonyeshi dalili yoyote.
Nao watumwa wale walipopokea mgao
wao, kila mmoja alifanya kama alivyoona ni vema machoni pake; aliyepokea talanta
tano akazifanyisha biashara na kupata faida ya zingine tano na aliyepokea mbili
vile vile akapata faida ya zingine mbili, ila, yule aliyepewa talanta moja
alichimba shimo nakuizika talanta ile mle dani. Fika hapa wapendwa,
ningalipenda kwanza tukumbuke somo la wiki jana, hasa pale tuliposoma kuhusu
vipawa vya Roho Mtakatifu, na jinsi mtu aliyepewa kipawa fulani, huwa pia anayomamlaka
juu ya kipawa kile. Kisa na maana ikiwa ni tabia ya mtumwa huyu aliyepewa talanta
moja na badala yake kuitumia anaamua kuizika katika ardhi hadi Bwana wake
atakaporudi ili amrejeshee. Hapa twafahamishwa kuwa kuna baadhi ya waumini watakaobarikiwa
na vipawa na kwa makusudi watakataa kutumia vipawa hivyo. Pili nataka tuone
hekima ya Bwana yule, yakuwa hakukosea kugawa kiasi kile alichowagawia kila
mmoja ya watumwa wake, maanake, kila mtumwa achuma faida kiasi sawa na kiwango alichogawiwa,
isipokuwa tu, yule wa talanta moja. Walakini nasisitiza kuwa huyo mtumwa
aliyepewa talanta moja, kwa upumbavu wake, yeye zaidi ya wenzake ndiye
anadhihirisha kuwa Bwana wao aliwajua watumwa wake vema, yaani, sio uweza wao
tu bali hata udhaifu wao pia aliujua na hili ndilo lamfanya kuwagawiya mali vile.
Naye Bwana yule aliporudi toka
safarini akaja kufanya hesabu ya mali yake, na watumwa wale wawili wa kwanza
wakajitokeza na kuthibitisha wema na uaminifu wao kwa Bwana wao kwa kumletea faida yote waliotengeza. Hapa najua baadhi yetu watajiuliza mbona
Bwana anakubali faida ilhali wiki jana tulisoma kuhusu wale wauza mafuta
(makuhani/ wachungaji) ambao Bwana mwenyewe aliwaita manabii wa uongo. Makuhani
wao hao aliwafananisha na mbwa mwitu wakali wanaovalia ngozi ya kondoo, sababu
ikiwa ni tamaa yao ya fedha na kwa ajili ya tamaa iyo hiyo wanapofika mbele
zake anawakemea na kuwakana kabisa! Ni kweli jambo hili laweza kukanganya kidogo,
lakini, ukitizama mifano yote miwili kwa makini hautapata shida kutofautisha
kati ya faida ya wale wauza mafuta na ya hawa watumwa. Tofauti kati yao
yadhihirika hivi; wale wauza mafuta walikuwa wakijitafutia faida yao wenyewe, hata
usiku ule Bwana harusi alipokuja hawakujitokeza kwenda kumlaki. Ilhali, hawa
watumwa wanajitokeza mbele za Bwana wao pindi tu anapowasili nakumpa faida yote
waliochuma, maanake, kujituma kwao kuliwa kwa lengo moja na lengo
hilo lilikuwa kumfurahisha Bwana wao kwa vyovyote vile ili atakapokuja wapate
kukubalika mbele zake, (2KOR. 5:4-10).
No comments:
Post a Comment