HAMMO GIZANI: MMEKUWA WANA WA NURU NA WANA WA MCHANA (SURA YA 4)
Neema
na iwe kwenu na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo.
Mungu Baba, tunakushukuru kwa ajili
ya wokozi na ukombozi uliotufanyia kwa kifo cha Mwanao wa kipekee, Bwana wetu
Yesu Kristo, ambaye ndiye mtangulizi wa vyote na katika yeye vyote viliumbwa
iwe, mamlaka, enzi, au usultani, vyote viliumbwa katika, yeye. Ewe, Bwana wetu tunakuhimidi
kwa kutufanya wana wa Mungu kwa kifo chako msalabani na kwa kufufuka kwako
ukawa malimbuko ya ufufuo na kutufanya tuwe mwili wako kwa uweza wa Roho wako
Mtakatifu. Ewe, Kichwa cha Kanisa, uliyetukomboa kwa gharama ya uhai wako
twaomba ututakase tena kwa Neno lako Takatifu na utujaze upya kwa Roho
Mtakatifu, ili tukaweze imarika katika imani na kuenenda kwa uaminifu na utiifu
tukizifuata nyayo zako siku zote za maisha yetu. Amin.
Wakristo wenzagu, kama ilivyo kawaida
yetu baada ya dua na kumtukuza Mungu, hufuata marudio ya yale tuliyosoma Juma
lililopita kwa kifupi. Kwenye Somo la Juma lililopita tulitilia manani umuhimu wa ubatizo kwa
Roho Mtakatifu, na mwongozo tulioufuata ulitokana na jibu lake Kichwa cha
Kanisa kwa wanafunzi wake. Wanafunzi walimwuliza Bw. Yesu, ni nini itakuwa dalili
ya kuja kwake na ya mwisho wa dunia? Naye alitabiri na kuwaeleza mambo mengi
yatakayotukia nyakati za mwisho, na katika jumla ya maelezo yake akawasimulia
mfano ule wa wanawali kumi. Mfano huu tuliuchambua kwa kina na kuona jinsi
Kristo Yesu alivyonena kwa mafumbo akieleza jinsi kuja kwake kutakavyo kuwa na
nini hasa ya wapasa watakatifu wake kufanya ili wakapate kukubalika kuingia
mbinguni pamoja naye, huko atakuwa tayari ameandaa karamu.
Basi bila kusita wala kulegeza
mwendo tutamalizia kuchambua mfano huo kwa kuangazia wauza mafuta. Kumbukeni
kuwa pale mwishoni mwa somo letu la wiki jana nilidokeza kuhusu wauza mafuta na
kusema kuwa wanaashiria makuhani/watumishi wa Mungu! Lakini kwanza hebu turejelee
jinsi ujio wa bwana harusi utakavyokuwa, (MAT. 25:5-6): “Hata bwana harusi
alipokawia, wote wakasinzia wakalala usingizi. Lakini usiku wa manane, pakawa
na elele. Haya bwana harusi; tokeni mwende kumlaki.” Kipengee hiki cha
tujulisha kuwa mwito ulitolewa kuwaamsha na kuwafahamisha wale wanawali waende
kumlaki bwana harusi maana alikuwa ameshawasili. Mwito huu ama sauti hii
itakuwa ya malaika mkuu atakayemtangulia BWANA kwa parapanda ya Mungu ili
kuwajulisha watakatifu wake watoke kwenda kumlaki, (1THE. 4:15-17). Walakini kama
tulivyoona kuna baadhi ya Wakristo ambao hawataruhusiwa kuingia harusini, Sawa na
wanawali wale tano wapumbavu waliopatikana kama hawajajitayarisha ipasavyo. Ikawa, badala yao kwenda kumlaki bwana harusi alipowasili iliwabidi watoke usiku huo wa
manane kwenda kusaka wauza mafuta ili wauziwe mafuta ya kuwasha taa zao. Ila waliporudi
harusini waliupata mlango ukiwa umefungwa, isitoshe, walipodai kufunguliwa,
bwana harusi aliwakomesha kwa kuwaambia, hawajui!
Tamko sawa na hili la bwana harusi
ambaye tulimtambua kuwa ni Bw. Yesu Kristo, la patikana (MAT. 7:23). Katika aya
hii ya saba ukianzia pale mwanzo, Kristo anafunza kuhusu unafiki na kufikia msatari
wa 15-20, anautahadharisha hadhira uwe macho kwa ajili ya wale awaitao manabii
wa uongo. Fika hapa najua kuna wale watakaotuhumu kuwa nimeanza kupotosha mada tunayozungumzia.
Nami nitakuulizeni, kama Kristo Yesu ndiye abatizaye kwa Roho, naye amefunga
milango, je, hao wauza mafuta waliobaki nje sawa na wale wanawali wapumbavu
wanafanya biashara halali? Tushikilie hapo kwanza huku tukirejelea yale Kristo
Yesu anaeleza kuwahusu hao manabii wa uongo, anasema, “tutawatambua kwa matendo
yao.” Kisha anafululiza kufafanua anachomanisha ili wewe na mimi pia tukaweze
kufaidika kwa kuwatambua na kuwaepuka kwa mapema. Ila cha kushangaza nikuwa anamalizia
kwa kusema watamjia siku ile na kusema; Bwana, Bwana, hatukufanya unabii, kufukuza
mapepo na hata kutenda miujiza mingi, kwa Jina lako. Naye atawakemea na kuwafukuza
watoke mbele zake licha ya shuhuda zao ambazo Bwana hakanushi! Hii ina maana
kuwa zile shuhuda ni za kweli. Lakini Bwana haridhii kuwakubali licha ya makuu
waliotenda kwa uweza wa Jina lake!
Wapendwa, mbona Kristo anawageuka
na kuwakemea watumishi wake? Kweli yeye mwenye haki anaweza kuwahukumu watu
wake vile? Kwa kweli hapa kuna wale watakaosema, “Hukumu aliyoitoa Bwana wetu si ya haki kamwe.” Walakini, ni nani
mwenye ufahamu wa mambo yote, hata yale ya siri adhaniyo mtu moyoni mwake, je,
si yeye yule mwenye haki. Hebu tufanye tendo la busara na kuchunguza hukumu hii
anayoitoa Bwana kwa watu waliofanya maajabu makuu kwa uweza wa Jina lake kwa
kutumia Maandiko Matakatifu. Bw. Yesu, alitutahadharisha kuhusu manabii wa
uwongo aliowataja kuwa mbwa mwitu wakali waliovalia ngozi ya kondoo na hata
shuhuda zao zitadhihirisha uweza wa Roho Mtakatifu katika huduma watakazo toa.
Kwa mujibu wa maelezo yake Bw. Yesu haitakuwa rahisi kuwatambua manabii wa
uongo, kwa kuwa watakuwa wamevalia ngozi ya kondoo na hivyo ukiwatazama kwa
macho watafanana kondoo, isitoshe, watakuwa na vipawa vya Roho maana watanena
kwa unabii, watawafukuza mapepo na kutenda miujiza si haba. Swali la
kujiuliza hapa ni, kama wanatenda haya yote kwa uweza wa Roho, dosari liko wapi
hata wakataliwe na Bwana waliyemtumikia?
Mtume Paulo katika waraka wake wa
kwanza kwa Wakorintho, anatujulisha kuwa roho wa unabii humtii nabii, (1KOR.
14:32-33). Hii inamaana kuwa Mungu humpa mtu kipawa, naye aliyekirimiwa kipawa
kile ana mamlaka juu ya kipawa alichopewa na jinsi atakavyo kitumia. Naye Mtume
Petro, ambaye alikuwa mmoja katika hadhira ile Kristo Yesu alipozungumza kuhusu
manabii wa uongo, katika waraka wake wa pili anatuonya vile vile; tujihadhari
na manabii wa uongo, (2 PET. 2:1-22). Mt. Petro katika maelezo yake anamtaja
Balaamu mwana wa Beori na jinsi alivyo karipiwa na Punda kwa ajili ya uhalifu
wake, (2 PET. 2:14-17). Balaamu kwa kweli alikuwa na kipawa cha unabii, yaani, alikuwa mtu aliye zungumziwa na Mungu moja kwa moja, na utabiri wake ulikuwa
wa kuaminika, (HES. 22-24). Ila, sawa na hao wanaomjia Bwana na kumweleza mambo
makuu waliyoyatenda kwa Jina lake, hakumridhisha Mungu aliyempa kipawa kile,
kwa kuwa matendo yake Balaamu hayakuambatana na makusudi ya Mungu juu ya watu
wake Israeli, aliolipwa kuwaroga. Ni uhalifu uo huo wa Balaamu, wakupenda fedha
unaoangaziwa na KristoYesu katika mfano wa wanawali kumi, maana, Bw. Yesu ndiye
hutubatiza kwa Roho Mtakatifu bure na kutugawia vipawa kwa mapenzi yake, (RUM.
5:1-5; 12: 6-9). Kwa hivyo yeyote auzaye mafuta ameanguka katika uhalifu wa
Balaamu kwa kutafuta ujira wa udhalimu, (MDO. 8:14-21; YUD. 11).
Wapenzi wa Mungu, la muhimu ni kujua
jinsi ya kuwatambua kwa uhakika hawa manabii wa uongo ili tuwaepuke na hukumu
yao itakapowajia isitupate sisi pamoja nao, (ISA. 24:1-3). Kumbukeni kuwa
Kristo, alianza kwa kutueleza tusihukumu ili nasi tusihukumiwe, hivi nikusema,
huwezi mrekebisha nduguyo ilhali wewe uko hatiani. Ujirekebishe kwanza ili ukaweze
kumrekebisha mwenzio, lau sivyo, uyatendayo ni sawa na unafiki, maana wewe
mwenye hatia kubwa zaidi (boriti) wajiona bora kuliko nduguyo mwenye kosa ndogo
(kibanzi) kukuliko, (MAT. 7:1-5). Ila, tukijihukumu kwanza na kujirekebisha
kweli kweli kwa kutoa boriti jichoni mwetu na hapo ndipo tutaweza kuona vema na
kuweza kukitoa kibanzi jichoni mwa ndugu zetu na wala hapatakuwa na
wakutuhukumu, (1KOR. 11:31).
No comments:
Post a Comment