Sunday, 7 September 2014

HAMMO GIZANI: MMEKUWA WANA WA NURU NA WANA WA MCHANA (SURA YA 1)



Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo.

 

Wapenzi na ndugu katika Kristo Yesu, tuliinue jina lake Muumba wa vyote kwa wingi wa karama zake maishani mwetu, hususan, sisi aliyotuzaa kwa asili ya Roho na moto. Kwa Roho Mtakatifu ametufanya upya; watu wasioongozwa na tamaa za mwili ambazo huishia mauti, bali watu wanaoongozwa kwa nia ya Roho ambayo huishia uzimani. Ametufanyia na amani katika Kristo Yesu, utimilifu wake Mwenyezi, Mungu Baba, asiyeonekana kwa macho. Tuzidishie Ewe, BWANA wetu wema na rehema zako ili tuijue na kuishika njia yako kwa uhakika, tukikutazamia kufunuliwa kwako. Amin.



Watakatifu kwa Neema ya Kristo Yesu, hadi sasa sidhani kama kuna ye yote ambaye tumeacha nyuma kuhusiana na mchakato mzima wa ‘Vipindi Saba Vya Neno La Mungu.’ Tumejadili mambo kadha wa kadha chini ya kichwa hiki kwa muda unaozidi majuma manne hadi sasa. Utaratibu huo umetuwezesha kuweka msingi thabiti wakutuwezesha kusoma na kuelewa chuo cha Ufunuo wa Yohana. Kitabu ambacho kinaogopwa na wengi nakutazamwa kama fumbo kubwa lisiloweza kufumbuliwa, hivi kwamba wengi wetu hatushughuliki kukisoma kabisa! 

 

Muda wake umetimia, kwa kuwa yaliyoandikwa kwa mafumbo enzi za kale Bwana ameyaweka wazi zamani hizi. Hebu nikuulizeni, enyi wateule zake Mungu Baba, ni Neno lipi, hata moja litokalo kinywani mwa Baba lafaa kukupita? kama jibu ni hakuna hata moja. Basi tujibidiisheni kukisoma, maana, aliyotaka tuyajue ameyaweka wazi, na zaidi anatuhimiza kulijua na kulitenda Neno lake. Sadfa na hayo, katika utangulizi wa chuo cha Ufunuo wa Yohana, baraka spesheli imeahidiwa ye yote awaye Yule atakaye soma na kuyashika yaliyoandikwa humo, (UFU. 1:3). 



Nafanya kurudia: fika hapa tumekuwa tukiangazia historia nzima ya ulimwengu tangu mwanzo hadi mwisho; Siku ya Kwanza hadi Siku ya Saba. Kati ya siku hizi, Siku ya Tano ndiyo tuliyoishughulikia kwa kina, maana, tulitambua siku hii ndiyo tuiishio kwa wakati huu. Kwa hiyo hatuna budi kuifahamu ili tusiishi sawa na watu wa mataifa pasi na kutathimini yanayotukia kila uchao au baadaye matokeo yatakuwa ya namna gani. Kama wenye hekima ya kweli kati ya wanadamu inatupasa zaidi sisi Wakristo kuwa macho na kufahamu vema zamani hizi tuiishio. Tukizingatia kuwa tunaabudu Mungu wa-kweli ambaye Yeye pekee anafahamu mambo yote kwa utimilifu; yaliyopita, yanayotendeka, na yatakayotokea, (ISA. 44:6-8).



Isitoshe, Mungu Baba katika Kisto Yesu ameipa Kanisa lake karama ya unabii, ili kuhami na mapema aila yake kabla hajatenda lolote. kwa kuwa kwanza huwajuza manabii zake alichoazimia kutenda nao hutueleza kuhusu makusudio ya Mola wetu, (UFU. 22: 6-7). Wala si hayo tu, Roho wa Mungu huchunguza yaliyomo moyoni mwa Mungu Baba na kuwajuza wateule zake, yaani, mimi na wewe ndugu katika Kristo. Sababu ikiwa kutuwezesha kuishi kwa utakatifu kama watu wa Mungu, ili tusifikwe na mambo kama watu wasio na ufahamu au hekima, (1KOR. 2:6-16).   

 

Basi Wakristo, njia siyo nyingine ila, ile ile, walioipitia ndugu zetu walio tutangulia akina; Musa, Yusufu, Daudi, Danieli, Ezra, Petro, Mathayo, Yohana, Paulo, na juu ya wote Bw. Yesu, Mwokozi na Mkombozi wetu sote. Yeye alituonesha kwa matendo mfano uliobora zaidi ya wote. Na mfano huu ndio desturi ya Mwili wake (Kanisa) kote kote duniani na katika historia na tamaduni za watakatifu wa Mungu. Desturi na tamaduni hii sio nyengine ila kuomba bila kukoma na kuenda katika utakatifu tukimtumainia Mungu kwa imani, daima.



Tukitimiza haya sawa na ndugu zetu kabla yetu, Mungu atatuzidishia karama zote za rohoni na kamwe hatutapungukiwa kwa lolote. Utiifu wetu kwa Neno Takatifu na kwa dua zetu mbele zake, hizi ndizo zana walizotumia wenzetu kabla yetu kwa mafanikio makuu na ndizo baado tunazohitaji katika kipindi hiki kilichojaa giza na maovu ya kila aina. Tusikate tamaa wapenzi wa Mungu maana Mungu ni upendo na hakuna ajuae kupenda zaidi yake, wala hakuna aliye na uwezo wakupigania wapenzi wake zaidi yake Mwenyezi, Bwana wa Majeshi, (ISA. 41:1-16). 

 

Tuseme nini zaidi wapenzi wa Mungu? Mie sioni lingine ila kijibidiisha katika Kulijua Neno Takatifu na kulitenda. Sawa na ushauri wa Mtume Paulo (1THES. 5:1-11), tukilijua Neno Takatifu tusilale usingizi kama wengine, bali tujivike kifuani imani na upendo na chapeo yetu iwe tumaini la wokovu. Kwa kuwa Mungu hakutuweka kwa hasira yake, bali tupate wokovu kwa Bwana wetu Yesu Kristo; ambaye alikufa kwa ajili yetu ili tuishi pamoja naye. Je, mwaona jinsi Mungu Baba alivyotufanya wandani wake? Basi tusijipunguzie karama iwayo yoyote ile. Tuzidi kutia bidii katika kumlingania Mungu Baba na kulisoma Neno Takatifu, maana, katika haya atatufunulia yote aliyotabiri kwa vinywa vya watakatifu wake na kutuandikia katika Biblia Takatifu. 

No comments:

Post a Comment