Monday, 22 September 2014

HAMMO GIZANI: MMEKUWA WANA WA NURU NA WANA WA MCHANA (SURA YA 3)



Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo.



Mungu Baba, Ewe, Muumba na Muumbuaji, twakuabudu na kunyenyekea mbele zako kwa ajili ya ukuu na uweza wako maishani mwetu. Tukikushukuru kwa yote unayotutendea, Ewe, usiye na hila wala uovu ndani yako, Baba mwema, unayetufahamisha makusudi yako kabla huja tenda jambo lolote. Daima mkweli na daima mwaminifu, Jalali, tuzidishie uwepo wako siku kwa siku ili tuweze kuukabili ulimwengu na maovu yake yote na zaidi tukaweze kukujua vema na kutembea nawe kwa imani hadidi tukiufuata uelekezi wako, Ewe, mchungaji mwema wa maisha yetu. Amin.



Wapenzi wa Mungu, enyi manukato yake Kristo Yesu, utimilifu wake Mungu Baba nawasabahi na kuwakaribisha katika somo la leo. Shabaha letu likiwa lile lile, kuzidi kujifunza Neno Takatifu la Mungu Baba yetu. Kama ilivyo desturi yetu, kwanza tutajikumbusha kwa kifupi yale tuliyosoma wiki jana; tulisoma kuhusu aliyekuwa Mfalme wa Yuda kwa jina Yosiah, na jinsi alivyotumika na Mungu kuwarejesha watu wake katika imani na ibada ya kweli. Kadhalika tuliona jinsi Mungu Baba alivyoahidi kumimina Roho wake kwa wote wenye mwili katika nyakati hizi za mwisho na kuwa atamuinua mtu atakaye tumika kama Mfalme Yosia alivyotumika, ili awatayarishe watakatifu wa Mungu wakaweze kumpokea Roho Mtakatifu atakapomiminwa. Jambo la msingi likiwa kuwawezesha watakatifu kujihami kiroho na kuimarika kiimani ili wakaweze kustahimili wakati mgumu utakaoifika dunia nzima sawa na Neno la Mungu wa Israeli alilozungumza kupitia vinywa vya manabii wake.



Somo la leo la ng’oa nanga kwa kuufuata mkondo ule tulioushika wiki jana na kuendelea kuchunguza umuhimu wa Roho Mtakatifu kumiminwa juu ya wote wenye mwili katika siku hizi za mwisho. Mwongozo wetu tunautoa toka mfano ule wa wanawali kumi, (MAT. 25: 1-13). Lakini, kabla ya kuuchambua mfano huu ni vema tuelewe kiini chake, yaani mbona Bw. Yesu akafunza vile na kusudi lake lilikuwa lipi kwa wasikilizaji wake. Ukirudi nyuma kidogo aya ya 24, hapo ndipo funzo nzima la anzia. Bw. Yesu atoka hekaluni na kuukwea mlima wa mizeituni ili apumzike, huku wanafunzi wake wakimwonyesha utukufu na ustadi wa Hekalu. Bali Bw. Yesu akawazungumzia na kubashiri yatakayojiri kwa muda usio mrefu, nao wakamwendea kwa faragha na kumuuliza awaeleze lini mambo hayo yote yatatendeka na nini dalili ya kuja kwake na ya mwisho wa dunia. Jibu alilowapa na maelezo yake yakajumuisha matukio mbali mbali yatakayo tendeka duniani kote katika nyakati za mwisho na akazidisha hata kuwanenea kwa mifano; mfano huu wa wanawali kumi na hata ule unaoufuata wa talanta ni katika jumla ya maelezo yake Kristo Yesu. Hata hivyo hatutashughulika na mfano huo wa talanta kwa sasa, lakini ifahamike kuwa sijamzuia mtu ye yote kujizulia baraka toka mfano huo, kwani Neno la Mungu liwazi kwetu sote.



Bila pingamizi, mfano huu wa wanawali kumi, q Bw. Yesu  aliunena ukiwa mojawapo kati ya maelezo yake alipolijibu lile swali aliloulizwa na wanafunzi wake kuhusu, nini dalili ya kuja kwake na ya mwisho wa dunia.  Kwa mukhutasari, katika mfano huu wa wanawali kumi, anaufananisha Ufalme wa mbinguni na sherehe ya harusi ambayo ikishaandaliwa bwana harusi akakawia kufika mpaka giza likaingia akiwa baado hajafika na hata waliokuwa wamejiweka tayari kumlaki wakalala. Cha muhimu ni kuwa sherehe haikuvunjwa na ijapokuwa bwana harusi alichelewa hatimaye aliwasili kukiwa usiku wa manane na kulakiwa na baadhi ya waliostahili kumlaki. Sababu ikiwa sio wote waliokuja harusini walikuwa wamejitayarisha vilivyo kwa sherehe, ilhali kwa kuzibeba taa zao yaonekana wote walikusudia kuwa bwana harusi angekawia kufika na hata kuchelewa hadi usiku umpate angali hajafika.



Fika hapa, nadhani ni wazi kwetu sote kuwa Bw. Yesu anaelezea mambo yaliyo nyeti sana tena kwa mafumbo, dhamira yake ikiwa ni kuwafunulia mambo yaliyositirika katika Roho wa Mungu kwa njia watakayoelewa kwa urahisi. Hivi ni kumaanisha kwamba, jibu alilowapa wandani wake na maelezo yale yaliwahusu moja kwa moja, kwani toka kwao Kanisa (Mwili wa Kristo), lilipata mafundisho yake Kristo; ambayo ndiyo msingi wa ibada, itikadi na kanuni za Ukristo. Msingi wa imani ya Ukristo ni kuwa tumaini tulionayo katika ukombozi wake Kristo Yesu utatimilika atakaporudi kuwachukuwa wote waliowake toka duniani na kuwapeleka mbinguni halafu ataihukumu dunia. Pasi na tumaini hii kuwepo katika imani ya Mkristo, bila shaka imani ile imepungukiwa, kwa kuwa imepuuza ushahidi mzima wa kufa na kufufuka kwake Mkombozi wetu Yesu Kristo. Maana, katika kifo na kufufuka kwake Mkombozi wetu alitimiza kazi yake ya kuukomboa ulimwengu na kuupatanisha na Mungu Baba na baada ya kufufuka alijidhihirisha kwa wanafunzi wake kisha akapaa juu mbinguni kwa ahadi kuwa atarudi tena (kama mwizi) kuwachukuwa wote waliowake ili wawe pamoja naye mahali alipo.



Mfano huu wa wanawali kumi, haswa, unaelezea ujio huu wa Bw. Yesu kama mwizi na jinsi watakatifu wake wanavyostahili kumsubiri yeye bwana harusi wakiwa wamejiandaa vilivyo, kwa kuwa ameandaa sherehe na hataghairi bali atakuja, hata kama atachelewa na kufika usiku katikati kwenye giza kuu lazima atakuja. Fika hapa ningependa tutilie maanani wanawali wale kumi. Tayari tumeona wanaashiria watakatifu wote wamwaminio KristoYesu, yaani, Kanisa, na ndio maana tunajulishwa kuhusu unawali/ubikra wao. Kwa hiyo hakuna sababu maalum yakutofautisha kati ya wale tano wenye busara na wale tano wapumbavu kwa msingi kuwa wale tano wa kwanza ndio wanaoashiria Kanisa ilhali wenzao wanaashiria walimwengu (watu wasio na imani katika Kristo Yesu). Hebu tutazame vema maelezo tunayopewa kuwahusu.



  • Wote kumi ni wanawali/mabikra

  • Wote kumi walialikwa sherehe kumlaki bwana harusi

  • Wote kumi walitwaa taa zao ila tano kati yao ndio walio twaa pamoja na mafuta katika vyombo vyao



Tokana na maelezo haya tunaona kuwa wote walikuwa watakatifu bila unajisi wo wote; ubikra,(2KOR. 11:2). Tena wote walikuwa wamealikwa katika sharehe ile kumlaki bwana harusi, hii ina maana kuwa walikuwa na ufahamu wa harusi ile na zaidi walikuwa maswahibu ama ukipenda wandani wake bwana harusi kwa lile jukumu waliloteuliwa kutimiza, yaani, kumlaki atakapowasili. Isitoshe wote walitwaa taa zao, kuonyesha walikusudia kuwa bwana harusi angelichelewa kwa kuwa hakuna aliyetamauka na kwenda, bali walimngoja hadi usiku wa manane, hii ina ashiria imani yao. Sawa na hayo, taa kama tujuavyo huashiria Neno Takatifu la Mungu, (ZAB.119:105) na mafuta huashiria Roho Mtakatifu, (KUT. 29:7; 1SAM. 16:13). Kama wote ni watakatifu na wateule zake bwana tena wenye imani kwake na wanalishika neno lake (taa), basi mbona baadhi yao (wale tano wapumbavu) hawakuruhusiwa kuingia harusini licha ya bidii yao na kujitolea kwao?



Wapendwa kama tulivyoona wote kumi walikuwa hali sawa isipokuwa kwa mafuta. Kama nikujitenga na ulimwengu na yote yanayoweza tia utakatifu wao najisi wote walifaulu. Kama ni kuwa na imani kuwa bwana harusi atakuja wote waliamini. Tushikilie hapo kwanza, na kutazama kuwa wote  ilifika pahali wakasinzia na kulala, maanake ni, imani ya kuwa bwana harusi atakuja ili didimia sawa na kukawia kwake kulivyo zidi; kukawia kule kunaashiria majaribu. Ila bwana harusi alipowasil na wote wakatoka nje kwenda kumlaki kuna wale kati yao hawakutwaa mafuta pamoja na taa zao kwa hiyo taa zao hazikuwaka. Kuzimika kwa taa zile kwa kukosa mafuta kunaashiria kupoteza imani na Neno la Mungu na badala yake kutegemea matendo  makavu pekee. Vile vile, kutokuwa na mafuta kunaashiria kutopokea ubatizo wa Roho Mtakatifu. Na huku kukosa mafuta ndio sababu ya taa zao kuzima na kutoweza kuwaka tena, hali kadhalika ikiwa ndiyo sababu yao kufungiwa nje na kutokubaliwa kuingia katika sherehe pamoja na bwana harusi. Kumbuka ilimfaa kila mmoja awe na mafuta chomboni mwake. Naye bwana harusi siye mwingine ila ni BWANA YESU KRISTO, (YN. 3:26-29).



Naye ndiye anayetueleza kupitia mfano huu kuhusu kuja kwake, ili tujiweke tayari kwa kutimiza yote yanayohusu imani na utakatifu. Na tunapofanya hivi isiwe kwa akili zetu tu na vile tunavyodhania mambo yatatukia, bali tumtegemee Roho Mtakatifu kutuangazia Neno lake hadi mwisho ili taa la tumaini letu lisizimike kwa kukosa mafuta wakati giza na majaribu yatakapozidi na Bwana wetu aonekane kukawia kuja, (YN. 16:13-15). Fika hapa, tunaona wazi kuna baadhi ya Wakristo watakaoachwa nyuma na Bwana atakapowakujia waliowake, (MAT. 7:21). Bali wapendwa isiwe hivyo kwetu sisi, nafasi baado tunayo hivi sasa kubadili mienendo yetu na hususan mtazamo wetu kuhusu Neno Takatifu; tuitisheni Roho Mtakatifu, na kutegemea uweza wake ili atuimarishe katika imani kwa kutuongoza katika kweli yote na kutupasha mambo yatakayotendeka hadi atapokuja BWANA YESU KRISTO kutuchukua. Na atakapokuja sisi tutamlaki kwa furaha, shangwe na nderemo maana atatupata tukiwa watimilifu kumpokea na  bila shaka atatukubalia kuingia pamoja naye mbinguni alikotuandalia sherehe, (UFU. 19:9).


  •  Sijazungumzia wanaouza mafuta, hawa ni makuhani/watumishi wa Mungu (ISA. 24:1-3; MAT. 7:21-23)

No comments:

Post a Comment