Sunday, 14 September 2014

HAMMO GIZANI: MMEKUWA WANA WA NURU NA WANA WA MCHANA (SURA YA 2)


Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo.

 

Mungu mwenye enzi ya milele na milele, tunakutukuza na kukushukuru kwa wema na rehema zako maishani mwetu. Maana, Ewe ndiwe Muumba wa vyote, iwe ni juu Mbinguni, hapa Duniani na Ulimwenguni mzima. Vyote vinavyoonekana na visivyoonekana viko chini ya uweza wako kwa kuwa vyote vinakuhitaji na kukutegemea Ewe, Mungu, Muumba na Muumbuaji. Isitoshe, hakuna kinacho weza kufananishwa nawe, kwa kuwa hauhitaji chotote au kumtegemea ye yote. Hauna mwanzo wala mwisho bali mwanzo na mwisho ni kazi yako Ewe, Alfa na Omega. Daima uhimidiwe na utukuzwe. Amin.


Tumejaliwa wiki nyingine na Bwana wetu, kwa hiyo tusilegee katika ibada na kumtumikia kwa mali zetu zote na katika kila hali, maana vyote tulivyo navyo ni vyake Yeye Karima, (RUM. 11:33-36). Kwanza tutarejelea somo la wiki jana kimukhtasari; tuwezaona umuhimu wa maombi na kusoma Biblia Takatifu kwa maisha ya mwanadamu na zaidi kwetu sisi Wakristo. Vile vile kuhakikisha kuwa kwa njia hii watakatifu wa kale walipata kujua mawazo ya Mola, na kuwezeshwa kutenda yaliyo sawa na mapenzi yake katika zamani zao. Sawa sawa na hayo tulitambua kwamba, hakuna njia mbadala kwetu sisi watakatifu wa zamani hizi ikiwa twataka kutenda mapenzi ya Mola wetu na kuhesabiwa haki mbele zake, (2TIM. 2:14-15; SEF. 2:3). Basi, enyi wapendwa katika Kristo Yesu, tuzidi jibidiisha katika njia hii tukiwakumbuka watakatifu wote aidha wawe wa madhehebu yetu au la, kwani sote tu viungo vya mwili mmoja (Kanisa) ambaye kichwa chake ni Kristo Yesu, (KOL. 1:13-18; 1KOR. 1:10-13).

 

Nasisitiza hivi kwa kuwa muda uliopo ni mfupi mno; saa ya kuja kwake Bw. Yesu kulichukua Kanisa lake imewadia! Walakini, Mkombozi wetu hatakuja bila kutuarifu na kutufanya tuwe tayari kwa ujio wake, sawa na enzi za kale Mungu alipotaka kutenda jambo kwanza aliwafahamisha watu wake. Aliwainua manabii kati yao na kuwapa karama na vipawa vya kila aina ili kuwafunza na kuwahubiria watu; wanyoshe njia zao na kuacha dhambi. Wajiweke tayari kwa ujio wa Mungu, aidha kwa rehema au hukumu. Mimi na wewe mpendwa hili ndilo jukumu letu katika kizazi hiki, tujitakase ili tupate kukubalika mbele za Mungu kwa maneno yetu pamoja na mwenendo wetu tuwafae wengi kwa kuwakumbusha utakatifu na utukufu wa Mungu. Wengi wakapate kuutazama mfano wetu na kumrudia Mungu Baba na kujengeka katika imani, huku tukiitazamia SIKU YA BWANA, (YOE. 2:17; 1PET. 2:9-10).

 

Wapendwa, msichukulie ni tashtiti wala kuchoshwa nakuhimiza kwangu; si ati sifahamu kuwa mambo haya ni ya msingi katika jumuiya nzima ya Wakristo, ila nawapeni tahadhari ya kwamba kila nabii aliyeitabiri SIKU YA BWANA alishinikiza kuwa yaja upesi! Sasa itakuwaje kwetu sisi ambao dalili zote zaonyesha kuwa enzi hii tuishio ndiyo waliotabiri kuihusu? Inatulazimu sote tunaompenda Kristo Yesu kwa nia moja tushirikiane kuimarisha mwili wa Kristo ko kote tuliko; nyumbani, shuleni, hata kazini, (2KOR. 5:1-10). Hasa, yatupasa kutambua yale Mungu Baba ameyaweka tayari kwa ajili ya watu wake katika kipindi hiki, ili tujihami  vilivyo na yatakayo ikuta dunia hii hivi karibuni kama tulivyoona katika masomo yaliyotangulia. Pia katika hayo tuliyosoma tulitambua zama hizi za leo za fanana zamani zile za Ufalme wa Yuda, kabla Mfalme Nebukadneza kuuvamia na kuupiga Ufalme ule kwa upanga. Na jinsi Mungu alivyofanya juu chini kupitia manabii wake ili awanusuru watu wake lakini wao walizidi kumkaidi hadi hukumu yake Mungu ilipowafikia sawa na yale aliyoyanena kwa vinywa vya manabii wake.

 

Kipindi hicho cha Ufalme wa Yuda kilichofanana na enzi hii yetu kilianza na umiliki wa Mfalme Manase. Mfalme huyu, aliijaza Nchi ya Yuda damu isiyo na hatia na kuwapotosha watu wa Mungu kwa kutenda kila aina ya maouvu mpaka kuleta sanamu hekaluni na kumtoa mwanawe kafara kwa hiyo sanamu papo hapo hekaluni!....... Eeh, sitayarudia yote tuliyozungumzia, ila nataka kuwakumbusheni katika kipindi hicho kuna Mfalme mmoja aliye tenda tofauti na matendo ya wenzake, enhe, si mwingine ni Mfalme Yosia. Yeye ndiye aliye haribu sanamu hizo za Mfalme Manase, na kutoa amri Hekalu likarabatiwe na ibada pamoja na matoleo ya kila siku ya rejeshwe kama hapo awali. Kupitia juhudi zake Yuda ikapata muamko mkuu wa imani na kumrudia Mungu wa Israeli. Kwa kifupi nasema hivi, sawa na vile tulivyoona enzi hiyo ya kale ikiwa kioo cha enzi hii ya leo, hivyo ndivyo twatarajia kutatendeka, (2FAL. 22-23).

 

Mungu atamwinua mtu atakaye tumika kuleta uamusho katika Kanisa lake kabla hajatekeleza hukumu yake duniani. Tofauti itakayokuwepo ni kuwa sote tutakaokuwa tumesafisha “nguo zetu” na kuwa safi tutashiriki katika uamusho huo. Uamusho huu ndio utatimiza kwa utimilifu neno lile alilolinena Nabii Yoeli kuhusu Roho wa Mungu kumiminwa juu ya wote wenye mwili kabla ya SIKU YA BWANA, (YOE. 2:28-32). Kanisa tujiwekeni tayari, Mungu anakusudia kutenda mambo makuu katika Mwili wa Kristo na kisha autumie kwa uweza na utukufu kuhubiri Ufalme wake kabla haja ihukumu dunia hii kwa moto. 

No comments:

Post a Comment