HAKUNA
MUNGU: Dhana hii si mpya imekuwepo tangu jadi! Zaburi
(Psalms), 14: 1
Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo
kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo.
Kwa
kweli sijui nianzie wapi! Kawaida sipendi kujihusisha na michakato ambayo ni
ovyo. Yaani haina msingi wala lengo lolote lile la manufaa katika jamii ila
kueneza upambavu na upotovu! Bali, nakuulizeni, je, ni jambo ndogo kufanya
dhihaka na kuchukulia upuzi ishara zote ambazo bayana zinatudhihirishia kuwa
Mungu yupo? Nakuulizeni tena; je, ni jambo ndogo?
Ati,
limbukeni wanashikana kuunda kikundi ambacho msingi na shabaha yake nikueneza
dhana hii hii pumbavu na potovu eti, HAKUNA
MUNGU! Ewe, Mwingi wa fadhila tafadhali tuepushe mbali na shari zako.
Jamani, kwani ni upeo upi huu au ngazi gani hii ya elimu, ambayo hawa chipukizi
wamezamia? Maanake hapa ni dhahiri kuwa wanahitajia maelezo mbadala.
Uzushi
huu, una malengo maalum! Usishangae baada ya muda tukapata kusikia kuhusu
ufadhili toka kwa makundi fulani ya ughaibuni na mialiko yakuturai tukahudhurie
vikao vilivyo andaliwa kwa mbwembwe nyingi na gharama kuu. Nia ikiwa sio nyingine,
bali, kuwatega na kuwanasa walio wepesi kiakili na wale ambao baado hawajafanya
azma madhubuti kufuata muundo fulani katika maisha yao. Itakuwaje basi; tufyate
midomo ama tufunge macho pamoja na kuziba masikio kwa dai ati, hii ni karne
ambayo uhuru wakujieleza upo, umetambulika na kuheshimika na wote! Mmmh! Kama
huo ndo mwelekeo basi haina budi kuujibu mchakato huu kwa mujibu wa kanuni hiyo
hiyo.
Kwa
neema na kudura zake Mwenyezi, tutaweza kuwaopoa toka upambavu huu uliokithiri
na kuwarejesheni katika akili razini na mtazamo wa maisha uliosawa na hali
halisi ya mambo. Hapa naigusia kanuni moja kuu, inayokubalika mia-fil-mia katika
fani zote za utafiti na uchanganuzi wa kielimu. Kanuni yaelezea kwamba, Kazi iwayo yoyote ile ya kiufundi lazima
iwe imefanywa kwa akili na kwa ajili ya lengo mahususi. Nitataja mambo mawili
pekee, baadhi ya mengi yaliyoko ili kufafanua kanuni hii;
Mandhari
na uhai hapa Duniani: Hivi sasa hakuna awezaye kupinga
uhodari uliopo katika mpangilio wa maumbile; milima, miti, visiwa, bahari,
jangwa, au nyika. Vyote kwa mujibu wa wanamazingira kama hayati Prof. Mama
Wangari Mathaai, ni muhimu na huchangia si haba katika kuwepo kwa uhai hapa
duniani. Maanake kila kiumbe kina umuhimu wake, manufaa yake na lengo maalum la
kuwepo. Je, tunapo tenda kinyume na kuhujumu mpangilio wa maumbile? hasara
iliyoje ambayo hutupata, kama vile ukataji miti kiholela………………
Mpangilio
wa sayari toka Zebaki (Mercury) hadi Utaridi (Pluto):
Kila moja ya sayari hizi huwa na majira yake na mzingo wake maalum unao zunguka
Jua; haya hutendeka pasipo hata sayari moja kukosea njia au kupitwa na masika
yake. Kama unamiliki Saa ya mkononi fungua nyuma ushuhudie majira ya saa yako yanavozunguka.
Je, utasema ufundi huo unaoutazama ulijiunda pasipo fundi wa aina yeyote?
Tazama
tu, vile ilivyo rahisi kudhibitisha ustadhi na ustadi wa Mwenyezi katika kazi
alizozifanya kwa hekima na uweza mkuu!
Natumhimidi Yeye aliye juu, na
kumsifu na kumheshimu Yeye aishiye milele; kwa maana enzi na mamlaka Yake ni ya
milele hadi milele na matendo Yake yote ni kweli, na njia Zake ni za adili. Na
atukuzwe
Bw. Yesu Kristo, Utimilifu wake Mungu wa Kweli ulimwenguni kote. Amin.
No comments:
Post a Comment