Meza
ya Bwana: Madhumuni ya itikadi hii kuwepo katika familia teule ya Wakristo.
Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo
kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo.
Kabla
ya kuzama katika mada yetu ya leo, najua vema kuwa Wakristo tuko na itikadi
zetu tofauti kulingana na madhehebu tunayoshiriki. Lakini, kati ya itikadi hizo
kunazo kadhaa ambazo hutimizwa na Mwili wote wa Kristo yaani Kanisa, baadhi
ikiwa: Ubatizo; Kukiri imani ya Mitume
(Apostle’s Creed); Kushiriki Meza ya Bwana na Ndoa.
Kama
tujuavyo kila umma, taifa, muungano, kampuni au dini huwa na desturi na itikadi
zake maalum. Vivyo hivyo, pia kwetu sisi tunao kiri imani ya Ukristo zipo
itikadi ama ukipenda Sakramenti teule ambazo lazima kila Mkristo atimize kwa
njia moja au nyingine; Sakramenti hizi bila shaka ni muhimu katika malezi,
ukuaji na uimarishwaji kiimani na maishani.
Basi,
bila kuchelewa tuingilieni mada yetu ya leo. Kisa na maana, picha hiyo ya dharau mlioweka katika ukuta wenu wa facebook Mmmh! Nakuulizeni picha hii (cover
photo) ndo yaonyesha uhuru wakujieleza? Si uchokozi huo! Si matusi hayo! Kama
kweli hakuna Mungu, mbona mnawashwa na shughuli zake? Mbona mna kufuru
(blaspheme)?
Enyi
mlio shadidi wa cheche za matusi na majitapo, nitawaelezeni nini maanake
kushiriki Meza ya Bwana. Kwa kifupi, kushiriki meza ya Bwana, nikuadhimisha
peupe kifo cha Bwana Yesu Kristo msalabani kwa ajili ya dhambi zetu Binadamu.
Fauka ya hayo, inahuisha kiroho na huleta faraja na baraka zisizoweza
kuelezeka. Na, je, kuna madhumuni mengine ya itikadi hii kuwepo katika familia
teule ya Wakristo? Kwa hikika ndio, na yafuatayo ni baadhi ya Maandiko yatakayo
tupatia mwongozo mwafaka kujadili itikadi hii kwa upana zaidi;
Hakika Ya Ufufuo: Yohana
(YN.) 6:52-54. Hapa Bw. Yesu akiwa katika hulka yake ya kuhubiri Ufalme wa
Mungu, wanaomskiza wanaanza kushindana kwa kutoelewa maneno yake. Lakini,
tazama ujasiri ulioje na hakika yake, kwa yale anayowaeleza! Labda walidhani
ameteguka ulimi, maana ulimi hauna mfupa au sivyo? La, hasha! Amin, amin,
kaisema mara mbili ili kusisitiza yanayomtoka kinywani ni ukweli mtupu pasipo
ati-ati wala wahaka wowote ule. Ni sharti, ule mwili wake na unywe damu yake
ili uwe na uzima ndani yako. Nayo siku ya mwisho itakapofika ufufuo utakuwa
haki yako.
Shibe Toka Mbinguni: (YN.
6:55-59). Huku mashindano yakiendelea katika umati ule, Bw. Yesu; mwalimu shadidi,
anatumia fursa hiyo ya sintofahamu kufafanua maneno yake. Wayahudi wale
walokuwa pale mbele zake, wanafahamu vema miujiza na ishara za Mungu na jinsi
zilivyo ambatana na mababa zao walipokombolewa toka utumwa huko Misri, ususan,
mkate ulioshuka toka mbinguni wakiwa njanguani. Bali, Bw. Yesu, anasema yeye
ndo chakula cha kweli tofauti na mkate ule, maana walokula mkate ule baado
walikufa. Lakini, “aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu,
nami hukaa ndani yake……..kadhalika naye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi.”
Kuna Baraka gani zaidi ya kupokezwa uzima wa milele na uwepo wa Mungu Baba kuwa
nawe daima?
Kuja kwa Ufalme wa Mungu:
(LK. 22:14-20). Kwanza natutazame mapenzi na ustarabu wake Bw. Yesu; ijapokuwa
anakusudia mateso yakutamausha, shauku na fahari yake kubwa ipo kwa wale
wandani wake! Ili kuwaondolea huzuni kabla na kuifanya imani yao dhabiti
anapanga maandalizi haya murwa, licha ya tabu na mauti inayomchungulia
mlangoni! Kusudi analolipa kipaumbele ni kuwapa ukakamavu na kuhifadhi imani ya
wale maswahiba wake. Ili mateso yatakapoanza wasijeona kana kwamba mambo
yamemzidi kwa lolote lile, la hasha! Bali madhila yatakayo mkuta ni sambamba na mpangilio wa Mungu Baba, ili
Ufalme wake ukaweze kuja na wote watakao timiza itikadi hii kwa mujibu wa
imani, wawe warithi wa Ufalme huo tukufu na takatifu.
Kuungama kifo chake hadi atakaporudi
tena: (1KOR. 11:23-26). “Mnifuate mimi kama mimi
ninavyomfuata Kristo,” hivi ndivyo Mtume Paulo anavyoanza aya hii ya 11.
Madhumuni yake nikuhakikisha Wakriso wanafahamu hatua zake Bw. Yesu na
kuzifuata timilifu. Katika swala la kushiriki Chakula hiki hatua ile ile Kristo
alokuwa nayo ni kutilia mkazo dhana ambayo hudhihirika dhahiri shahiri kwa wote
kila wakati Wakristo wanapotimiza itikadi hii; dhana hii sio nyingine, ila
kuungama kifo chake Bw. Yesu, kwa ajili ya dhambi na utarajio ulioko moyoni mwa
washirika kuwa atarudi tena.
Hukumu:
(1KOR. 11:27-32). Hapa Mtume anawatahadharisha washirika wale tokana na tabia
zao mbovu zinazoshushia Meza ya Bwana hadhi na heshima inayostahiki. Kwa kuja
na kujishibisha matonge ya mikate na kubugia vikombe mpaka wakalewa chakari,
ilhali wenzao wabaki njaa! Zaidi, utovu huu wa nidhamu ambao unakaidi heshima
na utakatifu wa Meza ya Bwana anaushirikisha na wale wasio weza kuupambanua
Mwili wa Kristo. Maanake yeyote ule ambaye ana fahamu Kristo ni nani na kazi alioifanya
hawezi katu kutenda vile. La kusononesha ni kuwa onyo hii pakubwa inalenga
Wakristo! Lakini dhamani yake ni kuwa lengo lake ni kutuepusha na hukumu itakayopata
dunia hii. Vile vile, onyo hii inawalenga wasioamini, maana, pasipo imani
huwezi pambanua Kristo ni nani na umuhimu wa kazi alioifanya!
Daima,
Wakristo tumshukuru Mwenyezi, kwa Agano Jipya. Maana, kwa wingi wa mapenzi,
wema na fadhila zake alitukomboa tokana na adhabu ya dunia hii. Ushirika huu
kwetu ni onyesho la imani yetu, kwake kipenzi chetu Bw. Yesu Kristo, kwa
kutudhamini sisi zaidi ya uhai wake mwenyewe. Amin.
No comments:
Post a Comment