IMANI YA KWELI NI KUFAHAMU NA KUTENDA NENO LAKE (SURA 1)
Neema na iwe kwenu na amani,
zitokazo kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo.
Enyi wateule zake Haki, Ewe, Mwenye uweza wote, juu mbinguni, hapa duniani, chini kuzimu na
ulimwenguni kote, kheri na fadhila zizidi kuwatangulia toka kwake Masihi wa
Mungu uyo huyo aliye Ufufuo na uzima. Hususan katika kipindi hiki ambacho sote
tunang’amua kuwa kimejaa changamoto tele nchini na dunia nzima. Tukichukulia
hatua toka chapisho lililotangulia; Zaburi 40, nivema kutangulia kumshukuru Mungu, bila
kuchelea kwa maana ametujalia neema zake ambazo ni za milele. Hebu tutafakari kwa kina yale
yamekuwa yakitokea nchini; uvamizi, mauaji ya kiholela, milipuko na
mashambulizi ya kigaidi, uhasama wa kisiasa na kwa ujumla utulivu kutupotea kwa
kila hali! Kijumla twaweza sema, hali ya taharuki, majonzi na kiwewe ilikuwa
imeigubiga mipaka yote ya taifa letu!
Licha ya giza kukaa kama
ingetufunika, ghafla nuru ya amani ikachomoza! Swali la msingi litupasalo
kujiuliza ususan sisi Wakristo ni:- nikipi hasa ambacho kilitendwa kwa mkono wa
mwanadamu ili utulivu uanze kurejea? kama kawaida hapa wengi watatapatapa kwa visingizio
vya kila aina na maelezo marefu yaliyosheheni misamiati utadhani ni mashindano
yakutwikwa taji la kujieleza kwa ufasaha kwa Kimombo. Bali kando na sokomoko
hizo zote aliye na macho hambiwi tazama, maanake, bila shaka ahsanta, zote
nikwake Mwingi wa Rehema. Yeye, Rahmani mwingi wa Huruma ndiye katupandisha toka
shimo la uharibifu na toka udongo wa utelezi. Enhe! Si kwa mkono wa yeyote ule ila kwa uweza wake
Mungu wa Kweli. Yeye karidhia kutuepusha na uharibifu kwa kusikia kilio cha
wanawe wateule; Wakristo. Bila kusitasita, itambulike bayana kuwa ni maombi ya
Wakristo, kwa kufunga na kuombea taifa hili huku tukimlilia na kumgoja Mungu Baba
kwa uvumilivu ndiyo yamefanya haya. (ZAB. 133; MAT. 18:18-20).
Wapendwa, tazameni makuu yanayotendeka Mwili wa Kristo; Kanisa, linapoamua kuenenda kwa umoja na kwa ujasiri wa imani! Kila wakati
tunapochukua hatua sawa na Neno Lake Muumba mambo hutengenea sambamba na ahadi
zake. Hivi ni kusema kwamba kama kweli tutamtegemea kwa kutimiza mapenzi yake
maishani mwetu kila siku basi hatuna budi kuuona uweza wake mkuu ukitushindania
kwa jambo lolote lile, (KUT. 6:6-7). Uhakika wa mambo ndio huo, na kama
tunatambua hivi, basi nini hasa huwa kinatukwaza
tusiendelee na moyo huo wa umoja na maombi? Na nilipi la busara kutenda ilitujiepushe
na majanga kama haya kutufika tena? Majibu ya kuridhisha na ushauri nasaha
hautopatikana kwengine ila kwa Neno lake.
Ni hapa tu, katika Biblia Takatifu pekee ndipo tiba ya magonjwa na matatizo yote
yapo. Basi nakuulizeni kwa nini kujitaabisha kwa kuzurura huku na huko? Badala yake tujichoshe na kuvunjika nyoyo huku tukiwa wakavu, tukichekwa hata
kudharauliwa na hao mahasidi wa imani yetu!
(ISA. 9:6). Sio bora zaidi tulivyotangulia
kufululiza kusimama mwambani pahala ambapo hatua zetu ziliimarishwa kwa ajili ya dua. Hivi sasa
nani hana wimbo midomoni akielezea utulivu ulorejea? Kama atupeavyo Jua
na Mvua, wema kwa wabaya, vilevile amani hutufikishia sote. Wapendwa, nafanya
kusisitiza ili tusikizane, maombi ndio hutufungulia mlango wa rehema na uweza
wake Mola, akisharidhia sala zetu kilicho salia ni sisi kuenenda kwa utiifu na
uadilifu. Naye
pasi na wasiwasi atazidi kudumisha Uwepo wake maishani mwetu, na hii ni bakara isiyo
na kifani; Ibrahimu ka’elimishwa vile na Musa katambua ndivyo, (MWA. 15:1; KUT.
33: 15-16). Je, kwetu sisi twatarajia tuwe tofauti na bado tuuone ushindi wake
ukitutangulia? Abadan katani, nakuhakikishieni haijawahi na haitawahi fanyika wala tusijidanganye
itatendeka kwetu sisi. Kwani tubora kuliko Ibrahimu swahiba yake Mwenyezi Mungu
au Nabii Musa aliyenena naye uso kwa uso? Haitupasi sisi zaidi Ee, wapendwa kulishika
na kulitegemea Neno Lake, maana kwetu sisi kupitia dhabihu takatifu ya Mwana
wake wa Pekee atuhakikishia ahadi zake zote ni “Ndio na Amina,” (2KOR. 1:18-19).
Natuzidi wateule wa Bwana, tuzidi kutembea
katika njia hii ambayo tumeikanyaga, kamwe hatutajuta sawa na hao ndugu zetu
walio tutangulia. Nikitamatisha, kwa mfano wake Utimilifu wa Mungu, huyo Mwamba
wa Milele, (MAT. 7:24-27),hapa anatutofautishia mwenye hekima na mpambavu ni nani. Na kudhihirika kwao kwaja
wakati masumbuko na majanga yanapowakabili. Hebu
tafakari: Je, ni yupi nyumae atapaaza sauti
na kusema, Bwana akatia wimbo mpya kinywani mwangu, ndio sifa zake Mungu wetu? Isitoshe,
nani bado itakapohitajika ataweza kusimama tisti mbele za waovu na wanaokufuru Jina lake
Mtakatifu wa Watakatifu akiwa na ushuhuda utakao wafanya wengi kuogopa na
kumtumaini Bwana?
No comments:
Post a Comment