IMANI YA KWELI NI KUFAHAMU NA KUTENDA NENO LAKE (SURA 2)
Neema na iwe kwenu na amani,
zitokazo kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo.
Ahimidiwe, Mungu Baba, juu mbinguni,
hapa duniani na ulimwenguni kote. Kwa kudura zake ametuwezesha kupatana tena katika
ukurasa huu, ili tukaweze kuzidi kuangazia yanayotukabili siku baada ya siku
kwa minajili ya kufahamu nyakati tunazoishi. Tukidurusu kwa ufupi; wiki jana tuelekezea
kurunzi kadhia ambazo zimekuwa zikiendelea hapa nchini na kuona jinsi Mwenyezi
anavyotilia manani maisha yetu, na kutuepusha na uharibifu mara tulipoinua
sauti zetu na kumlilia. Ahsante, zetu kwa fadhila zako Baba wa mbinguni.
Walakini tusiache kufunga na kuomba hadi nchi yote itakapotulia tuli. Leo hii tutaendeleza
mchakato wetu wa “imani ya kweli,” huku tukilenga kujinasua tokana na kasumba
ya kutumainia mali.
Mwongozo wetu wa maisha kama
desturi na itikadi ya Kikristo hutoka kwa Neno Tukufu la Muumba wa vyote:-
Biblia Takatifu. Zaburi 49, sawa na chapisho la wiki ilopita ndio inatupa mwelekeo
ufaao kwa mchakato huu. Wapendwa, sote twajua kuwa mali au utajiri una
ushawishi mkuu tena wengi hushindwa kustahimili mshawasha wake kiasi cha
kupoteza nafasi zao katika makao ya milele, MT. 19:16-24. Kunena hivi
haimanishi tuchukulie aliyejari sawa na mtu aliyepotea, asilani! Utajiri ni
Baraka toka kwake Karima anyegawia wote kwa hekima zake. Bali kufanya mali kuwa
tegemeo na tumaini hapo ndipo mja hupotoka, LK. 12:13-21. Fika hapa najua wengi
watasema mambo haya twajua vema. Nami nitawaulizeni kweli mwafahamu?
Kuuliza vile si kejeli bali nikutoa
ilani ya mambo yanayotusibu! Wakristo hebu tujirudi wenyewe natuone jinsi Mwili
wa Kristo (Kanisa) ulivyo adhirika kwa kuegemea mali, vilevile, serikali na
asasi za utawala. Pakubwa mali na utajiri umefanywa chanzo cha kuheshimika na
kukubalika katika jamii. Nao wenye mali wamekuwa ndio washauri wakutamanika na
kuaminika, bora unacho utategewa sikio na kulimbikiziwa sifa sufufu. Fauka ya
hayo utakwezwa na kufanywa kielelezo cha wengi licha ya utovu wa maadili na
hata zaidi kukosa imani! Wahenga kamwe hawakukosea waliponena mavi ya tajiri
hayanuki.a
Mambo haya kama tujuavyo yamechangia
changamoto na taabu si haba katika Kanisa pamoja na utawala wa nchi; ushawishi
mkubwa unaotukabili ukitokana na nchi tajiri duniani na zenye uwezo. Sio siri
kuwa nchi hizi zimejizatiti kueneza na kufadhili upotovu na uovu wa kila aina
duniani kote. Ole, wetu sisi wanyonge tutakapo acha mwongozo wa Biblia Takatifu
na kushika mafunzo yao: Talaka; Usenge na Usagaji; Uafyaji Mimba; Uasi Mungu,
ni baadhi ya uchafu unaopaliliwa duniani na hao matajiri wenye uwezo, na
kubatizwa maisha ya kisasa. Bali wakristo tusichoke kuenenda katika uvumilivu
na unyenyekevu mwishowe Mungu wetu atatufariji, MT. 5:1-13; LK. 6:20-26.
Ijapokuwa tutafinyika tunahakika kwa
kinywa cha Kristo mwisho wetu ni mwema, tofauti na hawa wanaoupotosha ulimwengu,
hao tusiwaogope wala kuzitamani njia zao, ZAB. 49:16-20.
Mbarikiwa ni ewe Mkristo unayejiwekea
akiba mbinguni kwa matendo ya adili pamoja na kukesha na kuomba huku ukimtarajia
Mkombozi, MT. 6:19-21; Lk. 19:11-27. Mwenyezi, aridhie kutunasua na uchu ya
mali, bali atuzidishie uwezo na kaida ya kuenenda tukiwa imara katika hatua
zetu tukifuata nyayo zake daima. Pamoja nakutenda haya tukumbukeni viongozi wetu
wa Kanisa na Taifa, tuwapeane kwake Mchungaji Mwema ili awaongoze kule kwema
kwa hekima na uweza. Zaidi tukumbukeni, hata katika taabu na majaribu ni vema
zaidi kumhimidi Mungu kuliko mwanadamu, ZAB. 49:5-15.
Natumhimidi Yeye aliye juu, na
kumsifu na kumheshimu Yeye aishiye milele; kwa maana enzi na mamlaka Yake ni ya
milele hadi milele na matendo Yake yote ni kweli, na njia Zake ni za adili. Na
atukuzwe
Bw. Yesu Kristo, Utimilifu wake Mungu wa Kweli ulimwenguni kote. Amin.
No comments:
Post a Comment