Sunday, 12 October 2014
Sunday, 5 October 2014
HAMMO GIZANI: MMEKUWA WANA WA NURU NA WANA WA MCHANA (SURA YA 5)
Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo.
Ewe, Muumba wa mbingu, dunia na ulimwengu wote, twaliiuna Jina lako tukufu na takatifu lililojaa uweza, na kukushukuru kwa wema na rehema zako maishaini mwetu. Ewe, Mungu uishie milele, twanyeyekea mbele zako tukiomba utujalie uwepo wako maishani mwetu na uweza wako katika yote yanayotukabili. Pia twakuomba utuzidishie rehema zako siku kwa siku kwa kuwa tuwakosaji, viumbe dhaifu ambao msingi wetu ni udongo sawa na fahari yote ya maisha yetu. Ewe, mwingi wa subira, tuongoze kwa neema na utufahamishe njia zako ili tuzipitie siku zote na kwa mwenendo wetu kulifanya Jina lako kutukuzwa na watu wote daima. Amin.
Wapendwa wa Kristo Yesu, kama ilivyo kawaida yetu tukishajipeana kwake Mungu Baba, nakuziendeleza sifa zake twazama katika kuangaza Neno Takatifu ili tuimarishe imani yetu kwa kujifahamisha mapenzi yake Bwana wetu kwetu sisi tunaotumai kumwona ana kwa ana siku isiyo mbali. Mungu Baba kwa mapenzi yake mwenyewe aliridhia kutupatanisha naye tena kwa ukombozi mkuu; ukombozi uliofanyika kwa kifo cha Mwana wake wakipekee Yesu Kristo. Na kwa kumwamini Yesu Kristo twapewa uweza wa kuwa wana wa Mungu, na warithi wa ufalme wake pamoja na Kristo Yesu aliye Mkombozi na Mwokozi wa wote. Yeye ndiye tunasubiri kufunuliwa kwake kama alivyotueleza ili tuwe pamoja naye milele hata milele. Kufunuliwa huku kukaribu mno na inatubidi tujitahidi kulijua Neno lake na kulishika kabisa ili siku itakapofika tusiwe wa kutahayari na kuachwa nyuma kama wale wanawali wapumbavu.
Ni hapo wiki jana tulichambua mfano huu wa wanawali kumi, katika uchambuzi wetu tuliona jinsi Bw. Yesu alivyoutumia kuwaeleza wanafunzi wake kwa mafumbo kuhusu kufunuliwa kwake. Dhamira yake ikiwa kuwapa tumaini la kweli kuwa watamwona tena na kuishi pamoja naye daima milele. Hata sisi tuliopo leo hii tuwashiriki wa tumaini ile sawa na wale waliomsikiliza aliponena mfano huu. Na kwa hakika utakubaliana nami kwamba kwa ukubwa shabaha yake Bw. Yesu alipotabiri kuja kwake kupitia mfano huu, ilikuwa ni sisi Wakristo tuishio katika nyakati hizi za mwisho, sawa na mfano unaoufuata wa Talanta, (MAT. 25:14-30). Mfano huu wa Talanta ndiyo tutaangazia katika somo letu la wiki hii. Na kwa kifupi, mfano huu unatueleza kuhusu Bwana mmoja aliye waita watumwa wake na kuwakabidhi mali zake; kila mmoja kwa kadiri ya uwezo wake, kisha Bwana huyo akafunga safari ya siku nyingi. Halafu muda mrefu ulipokwisha Bwana yule alirejea na kufanya hesabu ya mali aliowapa watumwa wake na kuwazawadia kila mmoja kwa kadri ya bidii yake. Ila tofauti na mfano wa wanawali, baada ya kuumaliza mfano huu Bw. Yesu, aliongeza maelezo yaliyofafanua mafumbo yake. Katika kufafanua mfano huu anaelezea vile Mwana wa Adamu atakavyokusanya mataifa mbele zake na kuwabagua, huku akiwakaribisha wale awaitao kondoo, waurithi ufalme wa Mungu na kuwafukuza wale awaitao mbuzi na kuwatupa katika moto wa milele.
Kabla hatujazama zaidi katika majadala wa leo ni vema kukumbuka kuwa mfano huu wa Talanta ndiyo unatamatisha jibu lake Bw. Yesu alipowajibu wanafunzi wake swali lao walipomwomba awajuze ni nini itakuwa dalili ya kuja kwake na ya mwisho wa dunia. Kwa hiyo, upambanuo wowote wa mfano huu lazima uwiane na maelezo yale mengine ambayo Bwana alitangulia kuwaeleza wanafuzi wake kuhusu ni nini itakuwa dalili ya kuja kwake na ya mwisho wa dunia. Sababu ya kusema hivi ni kuwa mfano huu hutumika visivyo, ususan, kuwatia vijana motisha kutambua talanta zao na kuzitumia kama njia ya kujinasua na umasikini kwa kujitafutia riziki pasi na kutegemea kazi za kuajiriwa. Sisemi kuwa hivi ni vibaya, la, ila nasema kuwa uelewa huo hauwiani na madhumuni yake Bwana wetu, ikizingatiwa swali alilokuwa akijibu aliponena mfano huu.
Natuutazame mfano wenyewe: Mfano unaazia mstari wa kumi na nne kwa maneno, ‘Maana ni mfano wa mtu atakaye kusafiri,’ swali la kujiuliza hapa ni, nini hiki ambacho kinafananishwa? Nalo jibu lake twalipata katika aya iyo hiyo katika mstari wa kwanza, ‘Ndipo ufalme wa mbinguni utafanana na,’ kwa mujibu wa mstari huu ni bayana kuwa Bw. Yesu, anaendeleza jibu lake kwa swali la wanafunzi wake na ndiyo maana haoni haja ya kujirudia neno kwa neno anapoanza kuwasimulia mfano huu. Naye mtu huyo atakaye kusafiri si mwingine ila ni Yesu Kristo mwenywe, na hili twajua kwa mujibu wa maelezo yale aliyoyatoa mara tu alipomaliza kusimulia mfano huu wa talanta; mstari wa thelathini na moja. Ila kwa wale watakao ushahidi zaidi kwamba Bw. Yesu ndiye mwana wa Adamu, someni; (MAT. 8:20; 12:6-8; 13:41-43, LK. 19:9-10;). Nao, watumwa wale wanatuashiria sisi tuliookoka kwa kumwamini Bwana Yesu Kristo; hapa najua kuna wale watakaouliza itakuwaje Bwana atufananishe na watumwa? Ee, kwa kweli jambo hili si la kushanganza wala kudunisha kwani hata Mitume walipenda kujitambulisha kama watumwa wa Kristo Yesu hasa Mtume Paulo, (RUM. 1:1). Nazo mali walizopewa kila mtu kadiri ya uweza wake za ashiria vipawa Vya Roho Mtakatifu ambavyo Bwana humgawia kila moja kwa hekima na mapenzi yake, (RUM. 12:1-9).
Japokuwa tushaona kuwa ni Bwana atukirimiaye vipawa kwa hekima na mapenzi yake. Ningependa tutazame mstari wa kumi na tano kwa makini zaidi, “Akampa mmoja talanta tano, na mmoja talanta mbili na mmoja talanta moja; kila mtu kwa kadiri ya uwezo wake; akasafiri.” Kwa mujibu wa mstari huu, kwanza aliwapa mali (vipawa) kisha akasafiri, walakini, kama tujuavyo vipawa vya Roho vilitambulikana baada ya Pentekoste; siku ambayo Roho Mtakatifu alishuka kama ndimi za moto nakutua juu ya vichwa vya Mitume (MDO. 2:1-4). Je, tutasema kuwa Bw. Yesu alikosea ama hakutilia manani maneno yake alipozungumza vile? Tukumbukeni kuwa kile Bw. Yesu anachokifanya hapa ni kutabiri na hata kama ni kwa mafumbo, matukio ya mambo yale yatakapotimia lazima yafuate utaratibu ule. Na kwa kuwa baadhi ya mambo yale yalitimia muda mfupi baadaye, twajua kwa uhakika kuwa yalitendeka sawa na utaratibu wa unabii huu. Kwani kabla ya Pentekoste Bw. Yesu alitangulia kuwabatiza wanafunzi wake kwa Roho Mtakatifu kwa kuwavuvia na kuwaambia, “Pokeeni Roho Mtakatifu,” (YN. 20:22). Basi tutasemaje kuhusu yaliyotukia siku ya Pentekoste! Yaliyotukia siku hiyo ya Pentekoste yalithibitisha aliyokuwa tayari ameyatenda Bwana, (MDO. 1:6-9). Hali kadhalika, lazima kila Neno katika Biblia Takatifu litimie kadiri ya utaratibu wa vile ambavyo Neno lile lilinenwa, isitoshe, hata wewe mpenzi wa Mungu kama alikuahidi jambo subiri tu, maana, lazima litatimia sawa na Neno lake, hata kama matukio yanayokukabili hayaonyeshi dalili yoyote.
Nao watumwa wale walipopokea mgao wao, kila mmoja alifanya kama alivyoona ni vema machoni pake; aliyepokea talanta tano akazifanyisha biashara na kupata faida ya zingine tano na aliyepokea mbili vile vile akapata faida ya zingine mbili, ila, yule aliyepewa talanta moja alichimba shimo nakuizika talanta ile mle dani. Fika hapa wapendwa, ningalipenda kwanza tukumbuke somo la wiki jana, hasa pale tuliposoma kuhusu vipawa vya Roho Mtakatifu, na jinsi mtu aliyepewa kipawa fulani, huwa pia anayomamlaka juu ya kipawa kile. Kisa na maana ikiwa ni tabia ya mtumwa huyu aliyepewa talanta moja na badala yake kuitumia anaamua kuizika katika ardhi hadi Bwana wake atakaporudi ili amrejeshee. Hapa twafahamishwa kuwa kuna baadhi ya waumini watakaobarikiwa na vipawa na kwa makusudi watakataa kutumia vipawa hivyo. Pili nataka tuone hekima ya Bwana yule, yakuwa hakukosea kugawa kiasi kile alichowagawia kila mmoja ya watumwa wake, maanake, kila mtumwa achuma faida kiasi sawa na kiwango alichogawiwa, isipokuwa tu, yule wa talanta moja. Walakini nasisitiza kuwa huyo mtumwa aliyepewa talanta moja, kwa upumbavu wake, yeye zaidi ya wenzake ndiye anadhihirisha kuwa Bwana wao aliwajua watumwa wake vema, yaani, sio uweza wao tu bali hata udhaifu wao pia aliujua na hili ndilo lamfanya kuwagawiya mali vile.
Naye Bwana yule aliporudi toka safarini akaja kufanya hesabu ya mali yake, na watumwa wale wawili wa kwanza wakajitokeza na kuthibitisha wema na uaminifu wao kwa Bwana wao kwa kumletea faida yote waliotengeza. Hapa najua baadhi yetu watajiuliza mbona Bwana anakubali faida ilhali wiki jana tulisoma kuhusu wale wauza mafuta (makuhani/ wachungaji) ambao Bwana mwenyewe aliwaita manabii wa uongo. Makuhani wao hao aliwafananisha na mbwa mwitu wakali wanaovalia ngozi ya kondoo, sababu ikiwa ni tamaa yao ya fedha na kwa ajili ya tamaa iyo hiyo wanapofika mbele zake anawakemea na kuwakana kabisa! Ni kweli jambo hili laweza kukanganya kidogo, lakini, ukitizama mifano yote miwili kwa makini hautapata shida kutofautisha kati ya faida ya wale wauza mafuta na ya hawa watumwa. Tofauti kati yao yadhihirika hivi; wale wauza mafuta walikuwa wakijitafutia faida yao wenyewe, hata usiku ule Bwana harusi alipokuja hawakujitokeza kwenda kumlaki. Ilhali, hawa watumwa wanajitokeza mbele za Bwana wao pindi tu anapowasili nakumpa faida yote waliochuma, maanake, kujituma kwao kuliwa kwa lengo moja na lengo hilo lilikuwa kumfurahisha Bwana wao kwa vyovyote vile ili atakapokuja wapate kukubalika mbele zake, (2KOR. 5:4-10).
Monday, 29 September 2014
HAMMO GIZANI: MMEKUWA WANA WA NURU NA WANA WA MCHANA (SURA YA 4)
Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo.
Mungu Baba, tunakushukuru kwa ajili ya wokozi na ukombozi uliotufanyia kwa kifo cha Mwanao wa kipekee, Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye ndiye mtangulizi wa vyote na katika yeye vyote viliumbwa iwe, mamlaka, enzi, au usultani, vyote viliumbwa katika, yeye. Ewe, Bwana wetu tunakuhimidi kwa kutufanya wana wa Mungu kwa kifo chako msalabani na kwa kufufuka kwako ukawa malimbuko ya ufufuo na kutufanya tuwe mwili wako kwa uweza wa Roho wako Mtakatifu. Ewe, Kichwa cha Kanisa, uliyetukomboa kwa gharama ya uhai wako twaomba ututakase tena kwa Neno lako Takatifu na utujaze upya kwa Roho Mtakatifu, ili tukaweze imarika katika imani na kuenenda kwa uaminifu na utiifu tukizifuata nyayo zako siku zote za maisha yetu. Amin.
Wakristo wenzagu, kama ilivyo kawaida yetu baada ya dua na kumtukuza Mungu, hufuata marudio ya yale tuliyosoma Juma lililopita kwa kifupi. Kwenye Somo la Juma lililopita tulitilia manani umuhimu wa ubatizo kwa Roho Mtakatifu, na mwongozo tulioufuata ulitokana na jibu lake Kichwa cha Kanisa kwa wanafunzi wake. Wanafunzi walimwuliza Bw. Yesu, ni nini itakuwa dalili ya kuja kwake na ya mwisho wa dunia? Naye alitabiri na kuwaeleza mambo mengi yatakayotukia nyakati za mwisho, na katika jumla ya maelezo yake akawasimulia mfano ule wa wanawali kumi. Mfano huu tuliuchambua kwa kina na kuona jinsi Kristo Yesu alivyonena kwa mafumbo akieleza jinsi kuja kwake kutakavyo kuwa na nini hasa ya wapasa watakatifu wake kufanya ili wakapate kukubalika kuingia mbinguni pamoja naye, huko atakuwa tayari ameandaa karamu.
Basi bila kusita wala kulegeza mwendo tutamalizia kuchambua mfano huo kwa kuangazia wauza mafuta. Kumbukeni kuwa pale mwishoni mwa somo letu la wiki jana nilidokeza kuhusu wauza mafuta na kusema kuwa wanaashiria makuhani/watumishi wa Mungu! Lakini kwanza hebu turejelee jinsi ujio wa bwana harusi utakavyokuwa, (MAT. 25:5-6): “Hata bwana harusi alipokawia, wote wakasinzia wakalala usingizi. Lakini usiku wa manane, pakawa na elele. Haya bwana harusi; tokeni mwende kumlaki.” Kipengee hiki cha tujulisha kuwa mwito ulitolewa kuwaamsha na kuwafahamisha wale wanawali waende kumlaki bwana harusi maana alikuwa ameshawasili. Mwito huu ama sauti hii itakuwa ya malaika mkuu atakayemtangulia BWANA kwa parapanda ya Mungu ili kuwajulisha watakatifu wake watoke kwenda kumlaki, (1THE. 4:15-17). Walakini kama tulivyoona kuna baadhi ya Wakristo ambao hawataruhusiwa kuingia harusini, Sawa na wanawali wale tano wapumbavu waliopatikana kama hawajajitayarisha ipasavyo. Ikawa, badala yao kwenda kumlaki bwana harusi alipowasili iliwabidi watoke usiku huo wa manane kwenda kusaka wauza mafuta ili wauziwe mafuta ya kuwasha taa zao. Ila waliporudi harusini waliupata mlango ukiwa umefungwa, isitoshe, walipodai kufunguliwa, bwana harusi aliwakomesha kwa kuwaambia, hawajui!
Tamko sawa na hili la bwana harusi ambaye tulimtambua kuwa ni Bw. Yesu Kristo, la patikana (MAT. 7:23). Katika aya hii ya saba ukianzia pale mwanzo, Kristo anafunza kuhusu unafiki na kufikia msatari wa 15-20, anautahadharisha hadhira uwe macho kwa ajili ya wale awaitao manabii wa uongo. Fika hapa najua kuna wale watakaotuhumu kuwa nimeanza kupotosha mada tunayozungumzia. Nami nitakuulizeni, kama Kristo Yesu ndiye abatizaye kwa Roho, naye amefunga milango, je, hao wauza mafuta waliobaki nje sawa na wale wanawali wapumbavu wanafanya biashara halali? Tushikilie hapo kwanza huku tukirejelea yale Kristo Yesu anaeleza kuwahusu hao manabii wa uongo, anasema, “tutawatambua kwa matendo yao.” Kisha anafululiza kufafanua anachomanisha ili wewe na mimi pia tukaweze kufaidika kwa kuwatambua na kuwaepuka kwa mapema. Ila cha kushangaza nikuwa anamalizia kwa kusema watamjia siku ile na kusema; Bwana, Bwana, hatukufanya unabii, kufukuza mapepo na hata kutenda miujiza mingi, kwa Jina lako. Naye atawakemea na kuwafukuza watoke mbele zake licha ya shuhuda zao ambazo Bwana hakanushi! Hii ina maana kuwa zile shuhuda ni za kweli. Lakini Bwana haridhii kuwakubali licha ya makuu waliotenda kwa uweza wa Jina lake!
Wapendwa, mbona Kristo anawageuka na kuwakemea watumishi wake? Kweli yeye mwenye haki anaweza kuwahukumu watu wake vile? Kwa kweli hapa kuna wale watakaosema, “Hukumu aliyoitoa Bwana wetu si ya haki kamwe.” Walakini, ni nani mwenye ufahamu wa mambo yote, hata yale ya siri adhaniyo mtu moyoni mwake, je, si yeye yule mwenye haki. Hebu tufanye tendo la busara na kuchunguza hukumu hii anayoitoa Bwana kwa watu waliofanya maajabu makuu kwa uweza wa Jina lake kwa kutumia Maandiko Matakatifu. Bw. Yesu, alitutahadharisha kuhusu manabii wa uwongo aliowataja kuwa mbwa mwitu wakali waliovalia ngozi ya kondoo na hata shuhuda zao zitadhihirisha uweza wa Roho Mtakatifu katika huduma watakazo toa. Kwa mujibu wa maelezo yake Bw. Yesu haitakuwa rahisi kuwatambua manabii wa uongo, kwa kuwa watakuwa wamevalia ngozi ya kondoo na hivyo ukiwatazama kwa macho watafanana kondoo, isitoshe, watakuwa na vipawa vya Roho maana watanena kwa unabii, watawafukuza mapepo na kutenda miujiza si haba. Swali la kujiuliza hapa ni, kama wanatenda haya yote kwa uweza wa Roho, dosari liko wapi hata wakataliwe na Bwana waliyemtumikia?
Mtume Paulo katika waraka wake wa kwanza kwa Wakorintho, anatujulisha kuwa roho wa unabii humtii nabii, (1KOR. 14:32-33). Hii inamaana kuwa Mungu humpa mtu kipawa, naye aliyekirimiwa kipawa kile ana mamlaka juu ya kipawa alichopewa na jinsi atakavyo kitumia. Naye Mtume Petro, ambaye alikuwa mmoja katika hadhira ile Kristo Yesu alipozungumza kuhusu manabii wa uongo, katika waraka wake wa pili anatuonya vile vile; tujihadhari na manabii wa uongo, (2 PET. 2:1-22). Mt. Petro katika maelezo yake anamtaja Balaamu mwana wa Beori na jinsi alivyo karipiwa na Punda kwa ajili ya uhalifu wake, (2 PET. 2:14-17). Balaamu kwa kweli alikuwa na kipawa cha unabii, yaani, alikuwa mtu aliye zungumziwa na Mungu moja kwa moja, na utabiri wake ulikuwa wa kuaminika, (HES. 22-24). Ila, sawa na hao wanaomjia Bwana na kumweleza mambo makuu waliyoyatenda kwa Jina lake, hakumridhisha Mungu aliyempa kipawa kile, kwa kuwa matendo yake Balaamu hayakuambatana na makusudi ya Mungu juu ya watu wake Israeli, aliolipwa kuwaroga. Ni uhalifu uo huo wa Balaamu, wakupenda fedha unaoangaziwa na KristoYesu katika mfano wa wanawali kumi, maana, Bw. Yesu ndiye hutubatiza kwa Roho Mtakatifu bure na kutugawia vipawa kwa mapenzi yake, (RUM. 5:1-5; 12: 6-9). Kwa hivyo yeyote auzaye mafuta ameanguka katika uhalifu wa Balaamu kwa kutafuta ujira wa udhalimu, (MDO. 8:14-21; YUD. 11).
Wapenzi wa Mungu, la muhimu ni kujua jinsi ya kuwatambua kwa uhakika hawa manabii wa uongo ili tuwaepuke na hukumu yao itakapowajia isitupate sisi pamoja nao, (ISA. 24:1-3). Kumbukeni kuwa Kristo, alianza kwa kutueleza tusihukumu ili nasi tusihukumiwe, hivi nikusema, huwezi mrekebisha nduguyo ilhali wewe uko hatiani. Ujirekebishe kwanza ili ukaweze kumrekebisha mwenzio, lau sivyo, uyatendayo ni sawa na unafiki, maana wewe mwenye hatia kubwa zaidi (boriti) wajiona bora kuliko nduguyo mwenye kosa ndogo (kibanzi) kukuliko, (MAT. 7:1-5). Ila, tukijihukumu kwanza na kujirekebisha kweli kweli kwa kutoa boriti jichoni mwetu na hapo ndipo tutaweza kuona vema na kuweza kukitoa kibanzi jichoni mwa ndugu zetu na wala hapatakuwa na wakutuhukumu, (1KOR. 11:31).
Monday, 22 September 2014
HAMMO GIZANI: MMEKUWA WANA WA NURU NA WANA WA MCHANA (SURA YA 3)
Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo.
Mungu Baba, Ewe, Muumba na Muumbuaji, twakuabudu na kunyenyekea mbele zako kwa ajili ya ukuu na uweza wako maishani mwetu. Tukikushukuru kwa yote unayotutendea, Ewe, usiye na hila wala uovu ndani yako, Baba mwema, unayetufahamisha makusudi yako kabla huja tenda jambo lolote. Daima mkweli na daima mwaminifu, Jalali, tuzidishie uwepo wako siku kwa siku ili tuweze kuukabili ulimwengu na maovu yake yote na zaidi tukaweze kukujua vema na kutembea nawe kwa imani hadidi tukiufuata uelekezi wako, Ewe, mchungaji mwema wa maisha yetu. Amin.
Wapenzi wa Mungu, enyi manukato yake Kristo Yesu, utimilifu wake Mungu Baba nawasabahi na kuwakaribisha katika somo la leo. Shabaha letu likiwa lile lile, kuzidi kujifunza Neno Takatifu la Mungu Baba yetu. Kama ilivyo desturi yetu, kwanza tutajikumbusha kwa kifupi yale tuliyosoma wiki jana; tulisoma kuhusu aliyekuwa Mfalme wa Yuda kwa jina Yosiah, na jinsi alivyotumika na Mungu kuwarejesha watu wake katika imani na ibada ya kweli. Kadhalika tuliona jinsi Mungu Baba alivyoahidi kumimina Roho wake kwa wote wenye mwili katika nyakati hizi za mwisho na kuwa atamuinua mtu atakaye tumika kama Mfalme Yosia alivyotumika, ili awatayarishe watakatifu wa Mungu wakaweze kumpokea Roho Mtakatifu atakapomiminwa. Jambo la msingi likiwa kuwawezesha watakatifu kujihami kiroho na kuimarika kiimani ili wakaweze kustahimili wakati mgumu utakaoifika dunia nzima sawa na Neno la Mungu wa Israeli alilozungumza kupitia vinywa vya manabii wake.
Somo la leo la ng’oa nanga kwa kuufuata mkondo ule tulioushika wiki jana na kuendelea kuchunguza umuhimu wa Roho Mtakatifu kumiminwa juu ya wote wenye mwili katika siku hizi za mwisho. Mwongozo wetu tunautoa toka mfano ule wa wanawali kumi, (MAT. 25: 1-13). Lakini, kabla ya kuuchambua mfano huu ni vema tuelewe kiini chake, yaani mbona Bw. Yesu akafunza vile na kusudi lake lilikuwa lipi kwa wasikilizaji wake. Ukirudi nyuma kidogo aya ya 24, hapo ndipo funzo nzima la anzia. Bw. Yesu atoka hekaluni na kuukwea mlima wa mizeituni ili apumzike, huku wanafunzi wake wakimwonyesha utukufu na ustadi wa Hekalu. Bali Bw. Yesu akawazungumzia na kubashiri yatakayojiri kwa muda usio mrefu, nao wakamwendea kwa faragha na kumuuliza awaeleze lini mambo hayo yote yatatendeka na nini dalili ya kuja kwake na ya mwisho wa dunia. Jibu alilowapa na maelezo yake yakajumuisha matukio mbali mbali yatakayo tendeka duniani kote katika nyakati za mwisho na akazidisha hata kuwanenea kwa mifano; mfano huu wa wanawali kumi na hata ule unaoufuata wa talanta ni katika jumla ya maelezo yake Kristo Yesu. Hata hivyo hatutashughulika na mfano huo wa talanta kwa sasa, lakini ifahamike kuwa sijamzuia mtu ye yote kujizulia baraka toka mfano huo, kwani Neno la Mungu liwazi kwetu sote.
Bila pingamizi, mfano huu wa wanawali kumi, q Bw. Yesu aliunena ukiwa mojawapo kati ya maelezo yake alipolijibu lile swali aliloulizwa na wanafunzi wake kuhusu, nini dalili ya kuja kwake na ya mwisho wa dunia. Kwa mukhutasari, katika mfano huu wa wanawali kumi, anaufananisha Ufalme wa mbinguni na sherehe ya harusi ambayo ikishaandaliwa bwana harusi akakawia kufika mpaka giza likaingia akiwa baado hajafika na hata waliokuwa wamejiweka tayari kumlaki wakalala. Cha muhimu ni kuwa sherehe haikuvunjwa na ijapokuwa bwana harusi alichelewa hatimaye aliwasili kukiwa usiku wa manane na kulakiwa na baadhi ya waliostahili kumlaki. Sababu ikiwa sio wote waliokuja harusini walikuwa wamejitayarisha vilivyo kwa sherehe, ilhali kwa kuzibeba taa zao yaonekana wote walikusudia kuwa bwana harusi angekawia kufika na hata kuchelewa hadi usiku umpate angali hajafika.
Fika hapa, nadhani ni wazi kwetu sote kuwa Bw. Yesu anaelezea mambo yaliyo nyeti sana tena kwa mafumbo, dhamira yake ikiwa ni kuwafunulia mambo yaliyositirika katika Roho wa Mungu kwa njia watakayoelewa kwa urahisi. Hivi ni kumaanisha kwamba, jibu alilowapa wandani wake na maelezo yale yaliwahusu moja kwa moja, kwani toka kwao Kanisa (Mwili wa Kristo), lilipata mafundisho yake Kristo; ambayo ndiyo msingi wa ibada, itikadi na kanuni za Ukristo. Msingi wa imani ya Ukristo ni kuwa tumaini tulionayo katika ukombozi wake Kristo Yesu utatimilika atakaporudi kuwachukuwa wote waliowake toka duniani na kuwapeleka mbinguni halafu ataihukumu dunia. Pasi na tumaini hii kuwepo katika imani ya Mkristo, bila shaka imani ile imepungukiwa, kwa kuwa imepuuza ushahidi mzima wa kufa na kufufuka kwake Mkombozi wetu Yesu Kristo. Maana, katika kifo na kufufuka kwake Mkombozi wetu alitimiza kazi yake ya kuukomboa ulimwengu na kuupatanisha na Mungu Baba na baada ya kufufuka alijidhihirisha kwa wanafunzi wake kisha akapaa juu mbinguni kwa ahadi kuwa atarudi tena (kama mwizi) kuwachukuwa wote waliowake ili wawe pamoja naye mahali alipo.
Mfano huu wa wanawali kumi, haswa, unaelezea ujio huu wa Bw. Yesu kama mwizi na jinsi watakatifu wake wanavyostahili kumsubiri yeye bwana harusi wakiwa wamejiandaa vilivyo, kwa kuwa ameandaa sherehe na hataghairi bali atakuja, hata kama atachelewa na kufika usiku katikati kwenye giza kuu lazima atakuja. Fika hapa ningependa tutilie maanani wanawali wale kumi. Tayari tumeona wanaashiria watakatifu wote wamwaminio KristoYesu, yaani, Kanisa, na ndio maana tunajulishwa kuhusu unawali/ubikra wao. Kwa hiyo hakuna sababu maalum yakutofautisha kati ya wale tano wenye busara na wale tano wapumbavu kwa msingi kuwa wale tano wa kwanza ndio wanaoashiria Kanisa ilhali wenzao wanaashiria walimwengu (watu wasio na imani katika Kristo Yesu). Hebu tutazame vema maelezo tunayopewa kuwahusu.
Wote kumi ni wanawali/mabikra
Wote kumi walialikwa sherehe kumlaki bwana harusi
Wote kumi walitwaa taa zao ila tano kati yao ndio walio twaa pamoja na mafuta katika vyombo vyao
Tokana na maelezo haya tunaona kuwa wote walikuwa watakatifu bila unajisi wo wote; ubikra,(2KOR. 11:2). Tena wote walikuwa wamealikwa katika sharehe ile kumlaki bwana harusi, hii ina maana kuwa walikuwa na ufahamu wa harusi ile na zaidi walikuwa maswahibu ama ukipenda wandani wake bwana harusi kwa lile jukumu waliloteuliwa kutimiza, yaani, kumlaki atakapowasili. Isitoshe wote walitwaa taa zao, kuonyesha walikusudia kuwa bwana harusi angelichelewa kwa kuwa hakuna aliyetamauka na kwenda, bali walimngoja hadi usiku wa manane, hii ina ashiria imani yao. Sawa na hayo, taa kama tujuavyo huashiria Neno Takatifu la Mungu, (ZAB.119:105) na mafuta huashiria Roho Mtakatifu, (KUT. 29:7; 1SAM. 16:13). Kama wote ni watakatifu na wateule zake bwana tena wenye imani kwake na wanalishika neno lake (taa), basi mbona baadhi yao (wale tano wapumbavu) hawakuruhusiwa kuingia harusini licha ya bidii yao na kujitolea kwao?
Wapendwa kama tulivyoona wote kumi walikuwa hali sawa isipokuwa kwa mafuta. Kama nikujitenga na ulimwengu na yote yanayoweza tia utakatifu wao najisi wote walifaulu. Kama ni kuwa na imani kuwa bwana harusi atakuja wote waliamini. Tushikilie hapo kwanza, na kutazama kuwa wote ilifika pahali wakasinzia na kulala, maanake ni, imani ya kuwa bwana harusi atakuja ili didimia sawa na kukawia kwake kulivyo zidi; kukawia kule kunaashiria majaribu. Ila bwana harusi alipowasil na wote wakatoka nje kwenda kumlaki kuna wale kati yao hawakutwaa mafuta pamoja na taa zao kwa hiyo taa zao hazikuwaka. Kuzimika kwa taa zile kwa kukosa mafuta kunaashiria kupoteza imani na Neno la Mungu na badala yake kutegemea matendo makavu pekee. Vile vile, kutokuwa na mafuta kunaashiria kutopokea ubatizo wa Roho Mtakatifu. Na huku kukosa mafuta ndio sababu ya taa zao kuzima na kutoweza kuwaka tena, hali kadhalika ikiwa ndiyo sababu yao kufungiwa nje na kutokubaliwa kuingia katika sherehe pamoja na bwana harusi. Kumbuka ilimfaa kila mmoja awe na mafuta chomboni mwake. Naye bwana harusi siye mwingine ila ni BWANA YESU KRISTO, (YN. 3:26-29).
Naye ndiye anayetueleza kupitia mfano huu kuhusu kuja kwake, ili tujiweke tayari kwa kutimiza yote yanayohusu imani na utakatifu. Na tunapofanya hivi isiwe kwa akili zetu tu na vile tunavyodhania mambo yatatukia, bali tumtegemee Roho Mtakatifu kutuangazia Neno lake hadi mwisho ili taa la tumaini letu lisizimike kwa kukosa mafuta wakati giza na majaribu yatakapozidi na Bwana wetu aonekane kukawia kuja, (YN. 16:13-15). Fika hapa, tunaona wazi kuna baadhi ya Wakristo watakaoachwa nyuma na Bwana atakapowakujia waliowake, (MAT. 7:21). Bali wapendwa isiwe hivyo kwetu sisi, nafasi baado tunayo hivi sasa kubadili mienendo yetu na hususan mtazamo wetu kuhusu Neno Takatifu; tuitisheni Roho Mtakatifu, na kutegemea uweza wake ili atuimarishe katika imani kwa kutuongoza katika kweli yote na kutupasha mambo yatakayotendeka hadi atapokuja BWANA YESU KRISTO kutuchukua. Na atakapokuja sisi tutamlaki kwa furaha, shangwe na nderemo maana atatupata tukiwa watimilifu kumpokea na bila shaka atatukubalia kuingia pamoja naye mbinguni alikotuandalia sherehe, (UFU. 19:9).
Sijazungumzia wanaouza mafuta, hawa ni makuhani/watumishi wa Mungu (ISA. 24:1-3; MAT. 7:21-23)
Subscribe to:
Posts (Atom)