Sunday, 15 June 2014

SI TANGAMANE NA WAASI MUNGU

Si Tangamane Na Waasi Mungu

Vikaragosi wa Jehanamu, daima mcha Mungu kwao adui,

Kwa matusi na majitapo hushtumu, wakijidai ati hao ndo wasomi

Wakijiona wenye hekima kumbe n'pumbavu,  yao adhabu wajibebea kifuani

Si tangamane na waasi Mungu, uzao wa Lusifa malaika aliyelaaniwa kawa shaitwani!

 

Mcha Mungu zidisha dua, matendo na mwenendo mwema ziwe kwako pete na mkufu

Usimwonee masikini na umkumbuke mjane na yatima, kauli mbiu toka kwake Mungu

Tenda wengine utakavyo kutendwa, mhimidi Mola wako baraka takujazia maradufu

Si tangamane na waasi Mungu, uzao wa Lusifa malaika aliyelaaniwa kawa shaitwani!

 

Epukeni gadhabu na hamaki za Mumba, kwa kutia akili na uadilifu katika kazi zenu

Rahmani ni mwingi wa wema na fadhila, usipuuze rehema zake kwa kujizulia hukumu

Kiburi kikikuongoza mwisho tafedheheka, dhambi ikiwa yako fahari mwisho Jehanamu

Si tangamane na waasi Mungu, uzao wa Lusifa malaika aliyelaaniwa kawa shaitwani!

 

Bado muda upo wakubadili yako njia, mgeukie Masihi ni mwepesi wa kurehemu

Kila uchao huzifanya upya zake rehema, n'mwingi wa neema haweki akiba ya kosa zetu

Jisalimishe kwake katu hatokukataa, hakuna linalomzidi usitie shaka muamini tu

Si tangamane na waasi Mungu, uzao wa Lusifa malaika aliyelaaniwa kawa shaitwani!

 

 


No comments:

Post a Comment